MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

Peter's Denial

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 26:69–75

  1. 69 Wakati huu Petro alikuwa amekaa nje uani. Mjakazi mmoja akamjia na kumwambia, “Wewe pia ulikuwa pamoja na Isa wa Galilaya.”
  2. 70 Lakini Petro akakana mbele yao wote akisema, “Sijui hilo usemalo.”
  3. 71 Alipotoka nje kufika kwenye lango, mjakazi mwingine alimwona, akawaambia watu waliokuwako, “Huyu mtu alikuwa pamoja na Isa Al-Nasiri.”
  4. 72 Akakana tena kwa kiapo akisema, “Mimi simjui huyo!”
  5. 73 Baada ya muda mfupi, wale waliokuwa wamesimama pale wakamwendea Petro, wakamwambia, “Hakika wewe ni mmoja wao, kwa maana usemi wako ni kama wao.”
  6. 74 Ndipo Petro akaanza kujilaani na kuwaapia, “Mimi simjui mtu huyo!” Papo hapo jogoo akawika.
  7. 75 Ndipo Petro akakumbuka lile neno Isa alilokuwa amesema: “Kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.” Naye akaenda nje, akalia kwa majonzi.

Mrk 14:66–72

  1. 66 Petro alipokuwa bado yuko chini uani, tazama akaja mmoja wa wajakazi wa kuhani mkuu.
  2. 67 Alipomwona Petro akiota moto, akamtazama sana, akamwambia, “Wewe pia ulikuwa pamoja na Isa, Mnasiri.”
  3. 68 Lakini Petro akakana, akasema, “Sijui wala sielewi unalosema.” Naye akaondoka kuelekea kwenye njia ya kuingilia.
  4. 69 Yule mjakazi alipomwona mahali pale, akawaambia tena wale waliokuwa wamesimama hapo, “Huyu mtu ni mmoja wao.”
  5. 70 Lakini Petro akakana tena. Baada ya muda kidogo wale waliokuwa wamesimama hapo karibu na Petro wakamwambia, “Hakika wewe ni mmoja wao, kwa maana wewe pia ni Mgalilaya!”
  6. 71 Petro akaanza kujilaani na kuwaapia, “Mimi simjui huyu mtu mnayesema habari zake!”
  7. 72 Papo hapo jogoo akawika mara ya pili. Ndipo Petro akakumbuka lile neno Isa alikuwa amemwambia: “Kabla jogoo hajawika mara mbili, utanikana mara tatu.” Akavunjika moyo, akalia sana.

Luk 22:54–62

  1. 54 Kisha wakamkamata Isa, wakamchukua, wakaenda naye hadi nyumbani mwa kuhani mkuu. Lakini Petro akafuata kwa mbali.
  2. 55 Walipokwisha kuwasha moto katikati ya ua na kuketi pamoja, Petro naye akaketi pamoja nao.
  3. 56 Mjakazi mmoja akamwona kwa mwanga wa moto akiwa ameketi pale. Akamtazama sana, akasema, “Huyu mtu pia alikuwa pamoja na Isa!”
  4. 57 Lakini Petro akakana, akasema, “Ewe mwanamke, hata simjui!”
  5. 58 Baadaye kidogo, mtu mwingine alimwona Petro akasema, “Wewe pia ni mmoja wao!” Petro akajibu, “Wewe mtu, mimi sio mmoja wao!”
  6. 59 Baada ya muda wa kama saa moja hivi, mtu mwingine akazidi kusisitiza, “Kwa hakika huyu mtu naye alikuwa pamoja na Isa, kwa maana yeye pia ni Mgalilaya.”
  7. 60 Petro akajibu, “Wewe mtu, mimi sijui unalosema!” Wakati huo huo, akiwa bado anazungumza, jogoo akawika.
  8. 61 Naye Bwana Isa akageuka, akamtazama Petro. Ndipo Petro akakumbuka lile neno ambalo Bwana alimwambia: “Kabla jogoo hajawika leo, utanikana mara tatu.”
  9. 62 Naye akaenda nje, akalia kwa majonzi.

Jhn 18:15–27

  1. 15 Simoni Petro pamoja na mwanafunzi mwingine walikuwa wakimfuata Isa. Huyu mwanafunzi mwingine alikuwa anafahamika kwa kuhani mkuu, hivyo aliingia uani kwa kuhani mkuu pamoja na Isa.
  2. 16 Lakini Petro alisimama nje karibu na lango. Ndipo yule mwanafunzi mwingine, aliyejulikana na kuhani mkuu, akazungumza na msichana aliyekuwa analinda lango, akamruhusu Petro aingie ndani.
  3. 17 Yule msichana akamuuliza Petro, “Je, wewe pia si mmoja wa wanafunzi wa mtu huyu?” Petro akajibu, “Sio mimi.”
  4. 18 Wale watumishi na askari walikuwa wamesimama wakiota moto wa makaa kwa sababu palikuwa na baridi, Petro naye alikuwa amesimama pamoja nao akiota moto.
  5. 19 Wakati huo kuhani mkuu akawa anamuuliza Isa kuhusu wanafunzi wake na mafundisho yake.
  6. 20 Isa akamjibu, “Nimekuwa nikizungumza waziwazi mbele ya watu wote. Siku zote nimefundisha katika masinagogi na Hekaluni, mahali Wayahudi wote hukusanyika. Sikusema jambo lolote kwa siri.
  7. 21 Mbona unaniuliza mimi maswali? Waulize wale waliosikia yale niliyowaambia. Wanajua niliyoyasema.”
  8. 22 Alipomaliza kusema hayo, mmoja wa askari aliyekuwa amesimama karibu naye akampiga Isa kofi usoni. Kisha akasema, “Je, hivyo ndivyo unavyomjibu kuhani mkuu?”
  9. 23 Isa akamjibu akasema, “Kama nimesema jambo baya, shuhudia huo ubaya niliousema. Lakini kama nimesema yaliyo kweli, mbona umenipiga?”
  10. 24 Ndipo Anasi akampeleka Isa kwa kuhani mkuu Kayafa, akiwa bado amefungwa.
  11. 25 Wakati huo Simoni Petro alikuwa amesimama akiota moto. Baadhi ya watu waliokuwepo wakamuuliza, “Je, wewe si mmoja wa wanafunzi wake?” Petro akakana, akasema, “Sio mimi.”
  12. 26 Mmoja wa watumishi wa kuhani mkuu, ndugu yake yule mtu ambaye Petro alikuwa amemkata sikio, akamuuliza, “Je, mimi sikukuona kule bustanini ukiwa na Isa?”
  13. 27 Kwa mara nyingine tena Petro akakana, naye jogoo akawika wakati huo huo.