MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

Jesus before Pilate

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 27:11–26

  1. 11 Wakati huo Isa akiwa amesimama mbele ya mtawala, mtawala akamuuliza, “Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi?” Isa akasema, “Wewe wasema hivyo.”
  2. 12 Lakini viongozi wa makuhani na wazee walipomshtaki, hakujibu neno.
  3. 13 Ndipo Pilato akamuuliza, “Je, husikii ni mambo mangapi wanayokushtaki nayo?”
  4. 14 Lakini Isa hakumjibu hata kwa shtaka moja, kiasi kwamba mtawala alishangaa sana.
  5. 15 Basi ilikuwa ni desturi ya mtawala kumfungua mfungwa mmoja aliyechaguliwa na umati wa watu wakati wa sikukuu.
  6. 16 Palikuwa na mfungwa mmoja mwenye sifa mbaya, aliyeitwa Baraba.
  7. 17 Hivyo umati wa watu walipokusanyika, Pilato akawauliza hao watu, “Mnataka niwafungulie yupi: Baraba au Isa aitwaye Al-Masihi?”
  8. 18 Kwa kuwa alitambua kwamba walikuwa wamemkabidhi Isa kwake kwa ajili ya wivu.
  9. 19 Pilato akiwa ameketi kwenye kiti cha hukumu, mkewe akampelekea ujumbe huu: “Usiwe na jambo lolote juu ya mtu huyu asiye na hatia, kwa kuwa leo nimeteseka sana katika ndoto kwa sababu yake.”
  10. 20 Lakini viongozi wa makuhani na wazee wakashawishi umati wa watu kwamba waombe Baraba afunguliwe, naye Isa auawe.
  11. 21 Mtawala akawauliza tena, “Ni yupi kati ya hawa wawili mnayetaka niwafungulie?” Wakajibu, “Baraba.”
  12. 22 Pilato akawaambia, “Basi nifanye nini na huyu Isa aitwaye Al-Masihi?” Wakajibu wote, “Msulubishe!”
  13. 23 Pilato akauliza, “Kwa nini? Amefanya kosa gani?” Lakini wao wakazidi kupiga kelele, wakisema, “Msulubishe!”
  14. 24 Pilato alipoona kwamba hawezi kufanya lolote, lakini badala yake ghasia zilikuwa zinaanza, akachukua maji, akanawa mikono yake mbele ya umati wa watu, akasema, “Sina hatia kwa damu ya mtu huyu, hili ni jukumu lenu!”
  15. 25 Watu wote wakajibu, “Damu yake na iwe juu yetu na juu ya watoto wetu!”
  16. 26 Basi akawafungulia Baraba. Lakini baada ya kuamuru Isa apigwe mijeledi, akamtoa ili asulubishwe.

Mrk 15:1–15

  1. 1 Asubuhi na mapema, viongozi wa makuhani, pamoja na wazee, walimu wa Torati na Baraza la Wayahudi lote, wakafikia uamuzi. Wakamfunga Isa, wakamchukua na kumkabidhi kwa Pilato.
  2. 2 Pilato akamuuliza, “Je, wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi?” Isa akajibu, “Wewe umesema.”
  3. 3 Viongozi wa makuhani wakamshtaki kwa mambo mengi.
  4. 4 Pilato akamuuliza tena, “Je, huna la kujibu? Tazama ni mashtaka mangapi wanayaleta juu yako.”
  5. 5 Lakini Isa hakujibu lolote, hivyo Pilato akashangaa.
  6. 6 Ilikuwa desturi wakati wa Sikukuu ya Pasaka kumfungulia mfungwa yeyote ambaye watu wangemtaka.
  7. 7 Wakati huo, mtu aliyeitwa Baraba alikuwa amefungwa gerezani pamoja na waasi wengine waliokuwa wametekeleza uuaji wakati wa maasi.
  8. 8 Umati ule wa watu wakamjia Pilato na kumwomba awafanyie kama ilivyokuwa desturi yake.
  9. 9 Pilato akawauliza, “Mnataka niwafungulie huyu mfalme wa Wayahudi?”
  10. 10 Kwa maana yeye alitambua kuwa viongozi wa makuhani walikuwa wamemtia Isa mkononi mwake kwa ajili ya wivu.
  11. 11 Lakini viongozi wa makuhani wakachochea umati ule wa watu wamwombe awafungulie Baraba badala yake.
  12. 12 Pilato akawauliza tena, “Basi mnataka nifanye nini na huyu mtu mnayemwita mfalme wa Wayahudi?”
  13. 13 Wakapiga kelele, wakisema, “Msulubishe!”
  14. 14 Pilato akawauliza, “Kwa nini? Amefanya kosa gani?” Lakini wao wakapiga kelele zaidi, wakisema, “Msulubishe!”
  15. 15 Pilato, akitaka kuridhisha umati ule wa watu, akawafungulia Baraba. Naye baada ya kuamuru Isa apigwe mijeledi, akamtoa ili asulubishwe.

Luk 23:1–25

  1. 1 Kisha umati wote wa watu wakainuka na kumpeleka Isa kwa Pilato.
  2. 2 Nao wakaanza kumshtaki wakisema: “Tumemwona huyu mtu akipotosha taifa letu, akiwazuia watu wasilipe kodi kwa Kaisari na kujiita ni Al-Masihi, mfalme.”
  3. 3 Basi Pilato akamuuliza Isa, “Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi?” Isa akajibu, “Wewe wasema.”
  4. 4 Pilato akawaambia viongozi wa makuhani na umati ule wote, “Sioni msingi wowote wa kumshtaki mtu huyu!”
  5. 5 Lakini wao wakakazana kusema, “Anawachochea watu kwa mafundisho yake katika Yudea yote, tangu Galilaya alikoanzia, hadi sehemu hii!”
  6. 6 Pilato aliposikia hayo akauliza kama huyo mtu alikuwa Mgalilaya.
  7. 7 Alipofahamu kwamba Isa alikuwa chini ya mamlaka ya Herode, akampeleka kwa Herode, ambaye wakati huo alikuwa pia Yerusalemu.
  8. 8 Herode alipomwona Isa alifurahi sana, kwa sababu kwa muda mrefu alikuwa amesikia mambo mengi kumhusu. Pia alitarajia kumwona akifanya miujiza kadha wa kadha.
  9. 9 Herode akamuuliza maswali mengi, lakini Isa hakumjibu lolote.
  10. 10 Wakati huo viongozi wa makuhani na walimu wa Torati walikuwa wakitoa mashtaka yao kwa nguvu sana.
  11. 11 Herode na askari wake wakamdhihaki Isa na kumfanyia mzaha. Wakamvika vazi zuri sana, wakamrudisha kwa Pilato.
  12. 12 Siku hiyo, Herode na Pilato wakapata urafiki; kabla ya jambo hili walikuwa na uadui kati yao.
  13. 13 Basi Pilato akawaita pamoja viongozi wa makuhani, viongozi wengine na watu,
  14. 14 akawaambia, “Ninyi mlimleta huyu mtu kwangu kana kwamba ni mtu anayewachochea watu ili waasi. Nimemhoji mbele yenu nami sikupata msingi wowote wa mashtaka yenu dhidi yake.
  15. 15 Wala Herode hakumpata na kosa lolote, ndiyo sababu amemrudisha kwetu. Kama mnavyoona, mtu huyu hakufanya jambo lolote linalostahili kifo.
  16. 16 Kwa hiyo nitaamuru apigwe mijeledi na kumwachilia.” [
  17. 17 Kwa kuwa ilikuwa lazima kuwafungulia mfungwa mmoja wakati wa Sikukuu.]
  18. 18 Ndipo watu wote wakapiga kelele kwa pamoja, “Mwondoe mtu huyu! Tufungulie Baraba!”
  19. 19 (Baraba alikuwa amefungwa gerezani kwa sababu ya maasi yaliyokuwa yametokea mjini, na kwa ajili ya uuaji.)
  20. 20 Pilato, akitaka kumwachia Isa, akasema nao tena.
  21. 21 Lakini wao wakaendelea kupiga kelele wakisema, “Msulubishe! Msulubishe!”
  22. 22 Kwa mara ya tatu, Pilato akawauliza, “Kwani amefanya kosa gani huyu mtu? Sikuona kwake sababu yoyote inayostahili adhabu ya kifo. Kwa hiyo nitaamuru apigwe mijeledi, na kisha nitamwachia.”
  23. 23 Lakini watu wakazidi kupiga kelele kwa nguvu, wakidai kwamba Isa asulubiwe. Hivyo, kelele zao zikashinda.
  24. 24 Kwa hiyo Pilato akatoa hukumu kwamba madai yao yatimizwe.
  25. 25 Akamfungua yule mtu aliyekuwa amefungwa gerezani kwa kuhusika katika uasi dhidi ya serikali na mauaji. Akamkabidhi Isa mikononi mwao, wamfanyie watakavyo.

Jhn 18:28–40

  1. 28 Ndipo viongozi wa Wayahudi wakamchukua Isa kutoka kwa Kayafa na kumpeleka kwenye jumba la kifalme la mtawala Mrumi. Wakati huo ilikuwa ni alfajiri. Ili kuepuka kuwa najisi kwa taratibu za ibada, Wayahudi hawakuingia ndani ya jumba kwa sababu walitaka kushiriki katika Pasaka.
  2. 29 Hivyo Pilato akatoka nje walikokuwa, akawauliza, “Mmeleta mashtaka gani kumhusu mtu huyu?”
  3. 30 Wao wakamjibu, “Kama huyu mtu hakuwa mhalifu, tusingemleta kwako.”
  4. 31 Pilato akawaambia, “Basi mchukueni ninyi mkamhukumu kwa kufuata sheria zenu.” Wayahudi wakamjibu, “Sisi haturuhusiwi kutoa hukumu ya kifo kwa mtu yeyote.”
  5. 32 Walisema hivyo ili yale maneno aliyosema Isa kuhusu kifo atakachokufa yapate kutimia.
  6. 33 Kwa hiyo Pilato akaingia ndani ya jumba la kifalme, akamwita Isa, akamuuliza, “Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi?”
  7. 34 Isa akamjibu, “Je, unauliza swali hili kutokana na mawazo yako mwenyewe, au uliambiwa na watu kunihusu?”
  8. 35 Pilato akamjibu, “Je, mimi ni Myahudi? Taifa lako mwenyewe na viongozi wa makuhani wamekukabidhi kwangu. Umefanya kosa gani?”
  9. 36 Isa akajibu, “Ufalme wangu si wa ulimwengu huu. Ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, wafuasi wangu wangenipigania ili nisitiwe mikononi mwa viongozi wa Wayahudi. Lakini kama ilivyo, ufalme wangu hautoki hapa ulimwenguni.”
  10. 37 Pilato akamuuliza, “Kwa hiyo wewe ni mfalme?” Isa akajibu, “Wewe wasema kwamba mimi ni mfalme. Kwa kusudi hili nilizaliwa, na kwa ajili ya hili nilikuja ulimwenguni: ili niishuhudie kweli. Mtu yeyote aliye wa kweli husikia sauti yangu.”
  11. 38 Pilato akamuuliza Isa, “Kweli ni nini?” Baada ya kusema haya Pilato akaenda nje tena, akawaambia wale viongozi wa Wayahudi waliomshtaki Isa, “Sioni msingi wowote wa kumshtaki mtu huyu.
  12. 39 Lakini ninyi mna desturi yenu kwamba wakati wa Pasaka nimwachie huru mfungwa mmoja mnayemtaka. Je, mnataka niwafungulie huyu ‘mfalme wa Wayahudi’?”
  13. 40 Wao wakapiga kelele, wakajibu, “Si huyu mtu, bali tufungulie Baraba!” Yule Baraba alikuwa mnyang’anyi.