Zaburi 99
1 Mwenyezi Mungu anatawala, mataifa na yatetemeke; anakalia kiti cha enzi katikati ya makerubi, dunia na itikisike.
2 Mwenyezi Mungu ni mkuu katika Sayuni; ametukuzwa juu ya mataifa yote.
3 Wanalisifu jina lako ambalo ni kuu na la kuogopwa: yeye ni mtakatifu!
4 Mfalme ni mwenye nguvu na hupenda haki, wewe umethibitisha adili; katika Yakobo umefanya yaliyo haki na sawa.
5 Mtukuzeni Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, na mkaabudu katika mahali pa kuwekea miguu yake; yeye ni mtakatifu.
6 Musa na Haruni walikuwa miongoni mwa makuhani wake, Samweli alikuwa miongoni mwa walioliitia jina lake; walimwita Mwenyezi Mungu, naye aliwajibu.
7 Alizungumza nao kutoka nguzo ya wingu; walizishika sheria zake na amri alizowapa.
8 Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, ndiwe uliyewajibu, kwa Israeli ulikuwa Mungu mwenye kusamehe, ingawa uliadhibu matendo yao mabaya.
9 Mtukuzeni Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, mwabuduni kwenye mlima wake mtakatifu, kwa maana Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, ni mtakatifu.