Zaburi 98

1 Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya, kwa maana ametenda mambo ya ajabu; kitanga chake cha kuume na mkono wake mtakatifu umemfanyia wokovu.

2 Mwenyezi Mungu ameufanya wokovu wake ujulikane na amedhihirisha haki yake kwa mataifa.

3 Ameukumbuka upendo wake na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli; miisho yote ya dunia imeuona wokovu wa Mungu wetu.

4 Mpigieni Mwenyezi Mungu kelele za shangwe, dunia yote, ipaze sauti kwa nyimbo za shangwe na vinanda;

5 mwimbieni Mwenyezi Mungu kwa kinubi, kwa kinubi na sauti za kuimba,

6 kwa tarumbeta na mvumo wa baragumu za pembe za kondoo dume: shangilieni kwa furaha mbele za Mwenyezi Mungu, aliye Mfalme.

7 Bahari na ivume na kila kilicho ndani yake, dunia na wote wanaoishi ndani yake.

8 Mito na ipige makofi, milima na iimbe pamoja kwa furaha,

9 vyote na viimbe mbele za Mwenyezi Mungu, kwa maana yuaja kuhukumu dunia. Atahukumu dunia kwa haki na mataifa kwa haki.