Zaburi 100

1 Mpigieni Mwenyezi Mungu kelele za shangwe, dunia yote.

2 Mwabuduni Mwenyezi Mungu kwa furaha; njooni mbele zake kwa nyimbo za shangwe.

3 Jueni kwamba Mwenyezi Mungu ndiye Mungu. Yeye ndiye alituumba, sisi tu mali yake; sisi tu watu wake, kondoo wa malisho yake.

4 Ingieni malangoni mwake kwa shukrani na katika nyua zake kwa kusifu, mshukuruni yeye na kulisifu jina lake.

5 Kwa maana Mwenyezi Mungu ni mwema na fadhili zake zadumu milele; uaminifu wake unadumu kwa vizazi vyote.