Ezekieli 15

1 Neno la Mwenyezi Mungu likanijia kusema:

2 “Mwanadamu, je, ni vipi mti wa mzabibu unaweza kuwa bora kuliko tawi la mti mwingine wowote ndani ya msitu?

3 Je, mti wake kamwe huchukuliwa na kutengeneza chochote cha manufaa? Je, watu hutengeneza vigingi vya kuning’inizia vitu kutokana na huo mti wake?

4 Nao baada ya kutiwa motoni kama nishati na moto ukateketeza ncha zote mbili na kuunguza sehemu ya kati, je, unafaa kwa lolote?

5 Kama haukufaa kitu chochote ulipokuwa mzima, je, si zaidi sana sasa ambapo hauwezekani kufanyishwa chochote cha kufaa baada ya moto kuuchoma na kuuacha majivu?

6 “Kwa hiyo hili ndilo asemalo Bwana Mungu Mwenyezi: Kama nilivyoutoa mti wa mzabibu miongoni mwa miti ya msituni kuwa nishati ya moto, hivyo ndivyo nitakavyowatendea watu wanaoishi Yerusalemu.

7 Nitaukaza uso wangu dhidi yao. Ingawa watakuwa wameokoka kwenye moto, bado moto utawateketeza. Nitakapoukaza uso wangu dhidi yao, ninyi mtajua kuwa Mimi ndimi Mwenyezi Mungu.

8 Nitaifanya nchi kuwa ukiwa kwa sababu wamekuwa si waaminifu, asema Bwana Mungu Mwenyezi.”