The Triumphal Entry
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 21:1–11
- 1 Walipokaribia Yerusalemu, wakafika Bethfage katika Mlima wa Mizeituni. Ndipo Isa akawatuma wanafunzi wake wawili,
- 2 akawaambia, “Nendeni katika kijiji kilicho mbele yenu, nanyi mtampata punda amefungwa hapo, na mwana-punda pamoja naye. Wafungueni na mniletee.
- 3 Mtu yeyote akiwasemesha lolote, mwambieni kwamba Bwana ana haja nao, naye atawaruhusu mwalete mara moja.”
- 4 Haya yalitukia ili litimie neno lililonenwa na nabii, aliposema:
- 5 “Mwambieni Binti Sayuni, ‘Tazama, mfalme wako anakuja kwako, ni mpole, naye amepanda punda, juu ya mwana-punda, mtoto wa punda.’ ”
- 6 Wale wanafunzi wakaenda, wakafanya kama Isa alivyokuwa amewaagiza.
- 7 Wakamleta yule punda na mwana-punda, nao wakatandika mavazi yao juu ya hao punda, naye Isa akaketi juu yake.
- 8 Umati mkubwa wa watu wakatandaza mavazi yao barabarani, na wengine wakakata matawi kwenye miti, wakayatandaza barabarani.
- 9 Wale umati wa watu waliomtangulia na wale waliomfuata wakapaza sauti na kusema, “Hosana, Mwana wa Daudi!” “Amebarikiwa yeye ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!” “Hosana juu mbinguni!”
- 10 Isa alipoingia Yerusalemu, mji wote ukataharuki, watu wakauliza, “Huyu ni nani?”
- 11 Wale umati wa watu wakajibu, “Huyu ni Isa, yule nabii kutoka Nasiri ya Galilaya.”
Mrk 11:1–11
- 1 Walipokaribia Yerusalemu, wakafika Bethfage na Bethania katika Mlima wa Mizeituni. Isa akawatuma wawili wa wanafunzi wake,
- 2 akawaambia, “Nendeni katika kijiji kilicho mbele yenu. Na hapo mtakapoingia kijijini, mtampata mwana-punda amefungwa hapo, ambaye hajapandwa na mtu bado. Mfungueni, mkamlete hapa.
- 3 Mtu yeyote akiwauliza, ‘Mbona mnamfungua?’ mwambieni, ‘Bwana anamhitaji, na atamrudisha hapa baada ya muda mfupi.’ ”
- 4 Wakaenda, wakampata mwana-punda amefungwa kando ya barabara, karibu na mlango wa nyumba.
- 5 Walipokuwa wanamfungua, watu waliokuwa wamesimama karibu wakawauliza, “Kwa nini mnamfungua huyo mwana-punda?”
- 6 Wakawajibu kama vile Isa alivyokuwa amewaagiza, nao wale watu wakawaruhusu.
- 7 Kisha wakamleta huyo mwana-punda kwa Isa na kutandika mavazi yao juu yake, naye akampanda.
- 8 Watu wengi wakatandaza mavazi yao barabarani, na wengine wakatandaza matawi waliyokuwa wamekata mashambani.
- 9 Kisha wale waliokuwa wametangulia mbele na wale waliokuwa wakifuata nyuma wakapaza sauti, wakisema, “Hosana!” “Amebarikiwa yeye ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!”
- 10 “Umebarikiwa ufalme unaokuja wa baba yetu Daudi!” “Hosana kwake yeye aliye juu!”
- 11 Isa akaingia Yerusalemu na kwenda Hekaluni. Akaangalia kila kitu kilichokuwamo, lakini kwa kuwa ilishakuwa jioni, akaenda zake Bethania pamoja na wale kumi na wawili.
Luk 19:28–40
- 28 Baada ya Isa kusema haya, alitangulia kupanda kwenda Yerusalemu.
- 29 Naye alipokaribia Bethfage na Bethania kwenye mlima ulioitwa Mlima wa Mizeituni, aliwatuma wanafunzi wake wawili, akawaambia,
- 30 “Nendeni katika kijiji kilichoko mbele yenu. Na mtakapokuwa mnaingia kijijini, mtampata mwana-punda amefungwa hapo, ambaye hajapandwa na mtu bado. Mfungueni, mkamlete hapa.
- 31 Kama mtu akiwauliza, ‘Mbona mnamfungua?’ Mwambieni, ‘Bwana anamhitaji.’ ”
- 32 Wale waliotumwa wakaenda, wakapata kila kitu kama Isa alivyowaambia.
- 33 Walipokuwa wanamfungua yule mwana-punda, wenyewe wakawauliza, “Mbona mnamfungua huyo mwana-punda?”
- 34 Wale wanafunzi wakajibu, “Bwana anamhitaji.”
- 35 Wakamleta kwa Isa, nao baada ya kutandika mavazi yao juu ya huyo mwana-punda, wakampandisha Isa juu yake.
- 36 Alipokuwa akienda, watu wakatandaza mavazi yao barabarani.
- 37 Alipokaribia mahali yanapoanzia miteremko ya Mlima wa Mizeituni, umati wote wa wafuasi wake wakaanza kumsifu Mungu kwa furaha kwa sauti kuu kwa ajili ya matendo yote ya miujiza waliyoyaona. Wakasema:
- 38 “Amebarikiwa mfalme ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!” “Amani mbinguni na utukufu huko juu sana.”
- 39 Baadhi ya Mafarisayo waliokuwamo miongoni mwa umati ule wa watu wakamwambia, “Mwalimu, waamuru wanafunzi wako wanyamaze.”
- 40 Isa akawajibu, “Nawaambia ninyi, kama hawa watanyamaza, mawe yatapaza sauti.”
Jhn 12:12–19
- 12 Siku iliyofuata umati mkubwa wa watu waliokuwa wamekuja kwenye Sikukuu walisikia kwamba Isa angekuja Yerusalemu.
- 13 Basi wakachukua matawi ya mitende, wakatoka kwenda kumlaki, huku wakipaza sauti wakisema, “Hosana!” “Amebarikiwa yeye ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!” “Amebarikiwa mfalme wa Israeli!”
- 14 Isa akamkuta mwana-punda, akampanda, kama ilivyoandikwa,
- 15 “Usiogope, ewe Binti Sayuni; tazama, mfalme wako anakuja, amepanda mwana-punda!”
- 16 Wanafunzi wake Isa mwanzoni hawakuelewa mambo haya. Lakini Isa alipotukuzwa, ndipo walipokumbuka kuwa mambo haya yalikuwa yameandikwa kwa ajili yake na alitendewa yeye.
- 17 Wale waliokuwepo Isa alipomwita Lazaro kutoka kaburini na kumfufua kutoka kwa wafu waliendelea kushuhudia.
- 18 Na kwa sababu walikuwa wamesikia kwamba alikuwa ametenda muujiza huu, umati wa watu wakaenda kumlaki.
- 19 Hivyo Mafarisayo walipoona hayo, wakaambiana, “Mnaona, hamwezi kufanya lolote. Angalieni, ulimwengu wote unamfuata yeye!”