MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

The Triumphal Entry

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 21:1–11

  1. 1 Walipokaribia Yerusalemu, wakafika Bethfage katika Mlima wa Mizeituni. Ndipo Isa akawatuma wanafunzi wake wawili,
  2. 2 akawaambia, “Nendeni katika kijiji kilicho mbele yenu, nanyi mtampata punda amefungwa hapo, na mwana-punda pamoja naye. Wafungueni na mniletee.
  3. 3 Mtu yeyote akiwasemesha lolote, mwambieni kwamba Bwana ana haja nao, naye atawaruhusu mwalete mara moja.”
  4. 4 Haya yalitukia ili litimie neno lililonenwa na nabii, aliposema:
  5. 5 “Mwambieni Binti Sayuni, ‘Tazama, mfalme wako anakuja kwako, ni mpole, naye amepanda punda, juu ya mwana-punda, mtoto wa punda.’ ”
  6. 6 Wale wanafunzi wakaenda, wakafanya kama Isa alivyokuwa amewaagiza.
  7. 7 Wakamleta yule punda na mwana-punda, nao wakatandika mavazi yao juu ya hao punda, naye Isa akaketi juu yake.
  8. 8 Umati mkubwa wa watu wakatandaza mavazi yao barabarani, na wengine wakakata matawi kwenye miti, wakayatandaza barabarani.
  9. 9 Wale umati wa watu waliomtangulia na wale waliomfuata wakapaza sauti na kusema, “Hosana, Mwana wa Daudi!” “Amebarikiwa yeye ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!” “Hosana juu mbinguni!”
  10. 10 Isa alipoingia Yerusalemu, mji wote ukataharuki, watu wakauliza, “Huyu ni nani?”
  11. 11 Wale umati wa watu wakajibu, “Huyu ni Isa, yule nabii kutoka Nasiri ya Galilaya.”

Mrk 11:1–11

  1. 1 Walipokaribia Yerusalemu, wakafika Bethfage na Bethania katika Mlima wa Mizeituni. Isa akawatuma wawili wa wanafunzi wake,
  2. 2 akawaambia, “Nendeni katika kijiji kilicho mbele yenu. Na hapo mtakapoingia kijijini, mtampata mwana-punda amefungwa hapo, ambaye hajapandwa na mtu bado. Mfungueni, mkamlete hapa.
  3. 3 Mtu yeyote akiwauliza, ‘Mbona mnamfungua?’ mwambieni, ‘Bwana anamhitaji, na atamrudisha hapa baada ya muda mfupi.’ ”
  4. 4 Wakaenda, wakampata mwana-punda amefungwa kando ya barabara, karibu na mlango wa nyumba.
  5. 5 Walipokuwa wanamfungua, watu waliokuwa wamesimama karibu wakawauliza, “Kwa nini mnamfungua huyo mwana-punda?”
  6. 6 Wakawajibu kama vile Isa alivyokuwa amewaagiza, nao wale watu wakawaruhusu.
  7. 7 Kisha wakamleta huyo mwana-punda kwa Isa na kutandika mavazi yao juu yake, naye akampanda.
  8. 8 Watu wengi wakatandaza mavazi yao barabarani, na wengine wakatandaza matawi waliyokuwa wamekata mashambani.
  9. 9 Kisha wale waliokuwa wametangulia mbele na wale waliokuwa wakifuata nyuma wakapaza sauti, wakisema, “Hosana!” “Amebarikiwa yeye ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!”
  10. 10 “Umebarikiwa ufalme unaokuja wa baba yetu Daudi!” “Hosana kwake yeye aliye juu!”
  11. 11 Isa akaingia Yerusalemu na kwenda Hekaluni. Akaangalia kila kitu kilichokuwamo, lakini kwa kuwa ilishakuwa jioni, akaenda zake Bethania pamoja na wale kumi na wawili.

Luk 19:28–40

  1. 28 Baada ya Isa kusema haya, alitangulia kupanda kwenda Yerusalemu.
  2. 29 Naye alipokaribia Bethfage na Bethania kwenye mlima ulioitwa Mlima wa Mizeituni, aliwatuma wanafunzi wake wawili, akawaambia,
  3. 30 “Nendeni katika kijiji kilichoko mbele yenu. Na mtakapokuwa mnaingia kijijini, mtampata mwana-punda amefungwa hapo, ambaye hajapandwa na mtu bado. Mfungueni, mkamlete hapa.
  4. 31 Kama mtu akiwauliza, ‘Mbona mnamfungua?’ Mwambieni, ‘Bwana anamhitaji.’ ”
  5. 32 Wale waliotumwa wakaenda, wakapata kila kitu kama Isa alivyowaambia.
  6. 33 Walipokuwa wanamfungua yule mwana-punda, wenyewe wakawauliza, “Mbona mnamfungua huyo mwana-punda?”
  7. 34 Wale wanafunzi wakajibu, “Bwana anamhitaji.”
  8. 35 Wakamleta kwa Isa, nao baada ya kutandika mavazi yao juu ya huyo mwana-punda, wakampandisha Isa juu yake.
  9. 36 Alipokuwa akienda, watu wakatandaza mavazi yao barabarani.
  10. 37 Alipokaribia mahali yanapoanzia miteremko ya Mlima wa Mizeituni, umati wote wa wafuasi wake wakaanza kumsifu Mungu kwa furaha kwa sauti kuu kwa ajili ya matendo yote ya miujiza waliyoyaona. Wakasema:
  11. 38 “Amebarikiwa mfalme ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!” “Amani mbinguni na utukufu huko juu sana.”
  12. 39 Baadhi ya Mafarisayo waliokuwamo miongoni mwa umati ule wa watu wakamwambia, “Mwalimu, waamuru wanafunzi wako wanyamaze.”
  13. 40 Isa akawajibu, “Nawaambia ninyi, kama hawa watanyamaza, mawe yatapaza sauti.”

Jhn 12:12–19

  1. 12 Siku iliyofuata umati mkubwa wa watu waliokuwa wamekuja kwenye Sikukuu walisikia kwamba Isa angekuja Yerusalemu.
  2. 13 Basi wakachukua matawi ya mitende, wakatoka kwenda kumlaki, huku wakipaza sauti wakisema, “Hosana!” “Amebarikiwa yeye ajaye kwa Jina la Mwenyezi Mungu!” “Amebarikiwa mfalme wa Israeli!”
  3. 14 Isa akamkuta mwana-punda, akampanda, kama ilivyoandikwa,
  4. 15 “Usiogope, ewe Binti Sayuni; tazama, mfalme wako anakuja, amepanda mwana-punda!”
  5. 16 Wanafunzi wake Isa mwanzoni hawakuelewa mambo haya. Lakini Isa alipotukuzwa, ndipo walipokumbuka kuwa mambo haya yalikuwa yameandikwa kwa ajili yake na alitendewa yeye.
  6. 17 Wale waliokuwepo Isa alipomwita Lazaro kutoka kaburini na kumfufua kutoka kwa wafu waliendelea kushuhudia.
  7. 18 Na kwa sababu walikuwa wamesikia kwamba alikuwa ametenda muujiza huu, umati wa watu wakaenda kumlaki.
  8. 19 Hivyo Mafarisayo walipoona hayo, wakaambiana, “Mnaona, hamwezi kufanya lolote. Angalieni, ulimwengu wote unamfuata yeye!”