The Man with a Withered Hand
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 12:9–14
- 9 Isa akaondoka mahali hapo, akaingia ndani ya sinagogi lao,
- 10 na huko alikuwepo mtu aliyepooza mkono. Wakitafuta sababu ya kumshtaki Isa, wakamuuliza, “Je, ni halali kuponya siku ya Sabato?”
- 11 Isa akawaambia, “Ni nani miongoni mwenu, mwenye kondoo wake ambaye huyo kondoo akitumbukia shimoni siku ya Sabato hatamtoa?
- 12 Mtu ana thamani kubwa kuliko kondoo. Kwa hiyo ni halali kutenda mema siku ya Sabato.”
- 13 Ndipo akamwambia yule mtu, “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha, nao ukaponywa ukawa mzima kama ule mwingine.
- 14 Lakini Mafarisayo wakatoka nje na kupanga njama ya kumuua Isa.
Mrk 3:1–6
- 1 Isa akaingia tena ndani ya sinagogi, na kulikuwa na mtu aliyepooza mkono.
- 2 Wakawa wanamwangalia waone kama atamponya huyo mtu siku ya Sabato, ili wapate sababu ya kumshtaki.
- 3 Isa akamwambia yule mtu mwenye mkono uliopooza, “Njoo hapa mbele ya watu wote.”
- 4 Kisha Isa akawauliza, “Je, ni lipi lililo halali siku ya Sabato: Ni kutenda mema au kutenda mabaya? Ni kuokoa maisha au kuua?” Lakini wao wakanyamaza.
- 5 Isa akawatazama kwa hasira watu waliomzunguka pande zote, akahuzunika sana kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao. Akamwambia yule mtu mwenye mkono uliopooza, “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha, nao ukawa umeponywa kabisa!
- 6 Kisha Mafarisayo wakatoka nje, nao wakaanza kufanya njama ya kumuua Isa wakishirikiana na Maherode.
Luk 6:6–11
- 6 Ikawa siku nyingine ya Sabato, Isa aliingia ndani ya sinagogi na akawa anafundisha. Huko palikuwa na mtu ambaye mkono wake wa kuume ulikuwa umepooza.
- 7 Mafarisayo na walimu wa Torati walikuwa wakitafuta sababu ya kumshtaki Isa. Kwa hivyo wakawa wanamwangalia sana ili waone kama ataponya katika siku ya Sabato.
- 8 Lakini Isa alijua mawazo yao, hivyo akamwambia yule mtu mwenye mkono uliopooza, “Inuka usimame mbele ya watu wote.” Hivyo yule mtu akainuka, akasimama mbele yao wote.
- 9 Ndipo Isa akawaambia wale walimu wa Torati na Mafarisayo, “Nawauliza ninyi, ni lipi lililo halali siku ya Sabato? Ni kutenda mema au kutenda mabaya? Ni kuokoa maisha au kuyaangamiza?”
- 10 Akawatazama watu wote waliokuwepo, kisha akamwambia yule mtu, “Nyoosha mkono wako!” Akaunyoosha, na mkono wake ukawa umeponywa kabisa.
- 11 Wale wakuu wakakasirika sana, wakashauriana wao kwa wao ni nini watakachomtendea Isa.