MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

The Crucifixion

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 27:32–44

  1. 32 Walipokuwa wakienda, wakakutana na mtu mmoja kutoka Kirene, jina lake Simoni, nao wakamlazimisha kuubeba ule msalaba.
  2. 33 Wakafika mahali palipoitwa Golgotha (maana yake ni Mahali pa Fuvu la Kichwa).
  3. 34 Hapo wakampa Isa divai iliyochanganywa na nyongo ili anywe; lakini alipoionja, akakataa kuinywa.
  4. 35 Walipokwisha kumsulubisha, wakagawana mavazi yake kwa kuyapigia kura. [Hili lilifanyika ili litimie neno lililonenwa na nabii, “Waligawa nguo zangu miongoni mwao na vazi langu wakalipigia kura.”]
  5. 36 Kisha wakaketi, wakamchunga.
  6. 37 Juu ya kichwa chake, kwenye msalaba, wakaandika shtaka lake hivi: Huyu ni Isa Mfalme wa Wayahudi.
  7. 38 Wanyang’anyi wawili walisulubiwa pamoja naye, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wa kushoto.
  8. 39 Watu waliokuwa wakipita njiani wakamtukana huku wakitikisa vichwa vyao,
  9. 40 na kusema, “Wewe ambaye utalivunja Hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe mwenyewe basi! Kama wewe ni Mwana wa Mungu, shuka msalabani.”
  10. 41 Vivyo hivyo, viongozi wa makuhani, walimu wa Torati pamoja na wazee wakamdhihaki, wakisema,
  11. 42 “Aliwaokoa wengine, lakini hawezi kujiokoa mwenyewe! Yeye ni mfalme wa Israeli! Ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini.
  12. 43 Anamwamini Mungu, basi Mungu na amwokoe sasa kama anamtaka, kwa maana alisema, ‘Mimi ni Mwana wa Mungu.’ ”
  13. 44 Hata wale wanyang’anyi waliosulubiwa pamoja naye wakamtukana vivyo hivyo.

Mrk 15:21–32

  1. 21 Mtu mmoja kutoka Kirene, jina lake Simoni, baba yao Iskanda na Rufo, alikuwa anaingia mjini kutoka mashambani, nao wakamlazimisha kuubeba ule msalaba.
  2. 22 Kisha wakampeleka Isa hadi mahali palipoitwa Golgotha (maana yake ni Mahali pa Fuvu la Kichwa).
  3. 23 Nao wakampa divai iliyochanganywa na manemane, lakini hakuinywa.
  4. 24 Basi wakamsulubisha, nazo nguo zake wakagawana miongoni mwao kwa kuzipigia kura ili kuamua ni gani kila mtu ataichukua.
  5. 25 Ilikuwa saa tatu asubuhi walipomsulubisha.
  6. 26 Tangazo likaandikwa la mashtaka dhidi yake lenye maneno haya: Mfalme wa Wayahudi.
  7. 27 Pamoja naye walisulubiwa wanyang’anyi wawili, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wa kushoto. [
  8. 28 Nalo andiko likatimizwa, lisemalo, “Alihesabiwa pamoja na watenda dhambi.”]
  9. 29 Watu waliokuwa wakipita njiani wakamtukana huku wakitikisa vichwa vyao na kusema, “Aha! Wewe ambaye utalivunja Hekalu na kulijenga kwa siku tatu,
  10. 30 basi shuka kutoka msalabani na ujiokoe mwenyewe!”
  11. 31 Vivyo hivyo, viongozi wa makuhani pamoja na walimu wa Torati wakamdhihaki miongoni mwao wakisema, “Aliwaokoa wengine, lakini hawezi kujiokoa mwenyewe!
  12. 32 Basi huyu Al-Masihi, huyu mfalme wa Israeli, ashuke sasa msalabani, ili tupate kuona na kuamini.” Wale waliosulubiwa pamoja naye pia wakamtukana.

Luk 23:26–43

  1. 26 Walipokuwa wakienda naye, wakamkamata mtu mmoja aitwaye Simoni Mkirene, aliyekuwa anapita zake kuingia mjini kutoka shambani. Wakambebesha msalaba, wakamlazimisha auchukue nyuma ya Isa.
  2. 27 Idadi kubwa ya watu wakamfuata Isa, wakiwamo wanawake waliokuwa wakimlilia na kumwombolezea.
  3. 28 Isa akawageukia, akawaambia, “Enyi binti za Yerusalemu, msinililie mimi bali jililieni ninyi wenyewe na watoto wenu.
  4. 29 Kwa maana wakati utafika mtakaposema, ‘Wamebarikiwa wanawake tasa, ambao tumbo zao hazikuzaa, wala matiti yao hayakunyonyesha!’
  5. 30 Ndipo “ ‘wataiambia milima, “Tuangukieni!” na vilima, “Tufunikeni!” ’
  6. 31 Kwa maana kama wamefanya hivi kwa mti mbichi, kwa mti mkavu itakuwaje?”
  7. 32 Watu wawili wahalifu walipelekwa pamoja na Isa ili wakasulubiwe.
  8. 33 Walipofika mahali paitwapo Fuvu la Kichwa, hapo ndipo walimsulubisha Isa pamoja na hao wahalifu, mmoja upande wake wa kuume, na mwingine upande wake wa kushoto.
  9. 34 Isa akasema, “Baba, wasamehe, kwa maana hawajui walitendalo!” Wakagawana nguo zake kwa kupiga kura.
  10. 35 Watu wakasimama hapo wakimwangalia, nao viongozi wa Wayahudi wakamdhihaki wakisema, “Aliokoa wengine! Ajiokoe mwenyewe basi, kama yeye ndiye Al-Masihi wa Mungu, Mteule wake.”
  11. 36 Askari nao wakaja, wakamdhihaki. Wakamletea siki ili anywe,
  12. 37 na wakamwambia, “Kama wewe ni mfalme wa Wayahudi, jiokoe mwenyewe.”
  13. 38 Kwenye msalaba juu ya kichwa chake, kulikuwa na maandishi haya: Huyu ndiye Mfalme wa Wayahudi.
  14. 39 Mmoja wa wale wahalifu waliosulubiwa pamoja naye akamtukana, akasema: “Wewe si ndiye Al-Masihi? Jiokoe mwenyewe na utuokoe na sisi.”
  15. 40 Lakini yule mhalifu mwingine akamkemea mwenzake, akasema, “Je, wewe humwogopi Mungu, wakati uko kwenye adhabu hiyo hiyo?
  16. 41 Sisi tumehukumiwa kwa haki kwa kuwa tunapata tunayostahili kwa ajili ya matendo yetu. Lakini huyu mtu hajafanya kosa lolote.”
  17. 42 Kisha akasema, “Isa, unikumbuke utakapokuja katika ufalme wako.”
  18. 43 Isa akamjibu, “Amin, nakuambia, leo utakuwa pamoja nami Paradiso.”

Jhn 19:16–27

  1. 16 Ndipo Pilato akamkabidhi Isa kwao ili wamsulubishe. Isa asulubishwa (Mathayo 27:32-44; Marko 15:21-32; Luka 23:26-43) Kwa hiyo askari wakamchukua Isa.
  2. 17 Isa, akiwa ameubeba msalaba wake, akatoka kuelekea mahali palipoitwa Fuvu la Kichwa (kwa Kiebrania ni Golgotha).
  3. 18 Hapo ndipo walipomsulubisha. Pamoja naye walisulubisha watu wawili, mmoja kila upande wake, naye Isa katikati.
  4. 19 Pilato akaamuru tangazo liandikwe na liwekwe juu kwenye msalaba wa Isa; likasema: Isa Al-Nasiri Mfalme wa Wayahudi.
  5. 20 Kwa kuwa mahali hapo Isa aliposulubiwa palikuwa karibu na mjini, Wayahudi wengi walisoma maandishi haya yaliyokuwa yameandikwa kwa lugha za Kiebrania, Kiyunani na Kilatini.
  6. 21 Viongozi wa makuhani wa Wayahudi wakapinga, wakamwambia Pilato, “Usiandike ‘Mfalme wa Wayahudi,’ bali andika kwamba mtu huyu alisema yeye ni mfalme wa Wayahudi.”
  7. 22 Pilato akawajibu, “Nilichokwisha kuandika, nimeandika!”
  8. 23 Askari walipokwisha kumsulubisha Isa, walichukua nguo zake wakazigawa mafungu manne, kila askari fungu lake. Ila walikubaliana wasilichane lile vazi lake kwa maana lilikuwa halina mshono, bali limefumwa tangu juu hadi chini.
  9. 24 Wakaambiana, “Tusilichane ila tulipigie kura ili kuamua ni nani atalichukua.” Hili lilitukia ili Maandiko yapate kutimizwa yale yaliyosema, “Wanagawana nguo zangu, na vazi langu wanalipigia kura.” Hayo ndiyo waliyoyafanya wale askari.
  10. 25 Karibu na msalaba wa Isa walikuwa wamesimama mama yake, na dada wa mamaye, na Mariamu mke wa Klopa, na Mariamu Magdalene.
  11. 26 Isa alipomwona mama yake mahali pale, na yule mwanafunzi aliyempenda akiwa amesimama karibu, Isa akamwambia mama yake, “Mama, huyu hapa ndiye mwanao.”
  12. 27 Kisha akamwambia yule mwanafunzi, “Nawe huyu hapa ndiye mama yako.” Tangu wakati huo yule mwanafunzi akamchukua mama yake Isa nyumbani mwake.