Peter's Confession of Christ
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 16:13–20
- 13 Basi Isa alipofika katika eneo la Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake, “Watu husema kwamba mimi Mwana wa Adamu ni nani?”
- 14 Wakamjibu, “Baadhi husema ni Yahya; wengine husema ni Ilya; na bado wengine husema ni Yeremia au mmoja wa manabii.”
- 15 Akawauliza, “Je, ninyi mnasema mimi ni nani?”
- 16 Simoni Petro akamjibu, “Wewe ndiwe Al-Masihi, Mwana wa Mungu aliye hai.”
- 17 Naye Isa akamwambia, “Heri wewe, Simoni Bar-Yona, kwa maana hili halikufunuliwa kwako na mwanadamu, bali na Baba yangu aliye mbinguni.
- 18 Nami nakuambia, wewe ndiwe Petro na juu ya mwamba huu nitajenga jumuiya ya wafuasi wangu, hata malango ya Kuzimu hayataweza kuwashinda.
- 19 Nitakupa funguo za ufalme wa mbinguni, na lolote utakalolifunga duniani litakuwa limefungwa Mbinguni, nalo lolote utakalofungua duniani litakuwa limefunguliwa mbinguni.”
- 20 Kisha akawakataza wanafunzi wake wasimwambie mtu yeyote kwamba yeye ndiye Al-Masihi.
Mrk 8:27–30
- 27 Isa na wanafunzi wake wakaelekea vijiji vya Kaisaria-Filipi. Walipokuwa njiani, Isa akawauliza, “Watu husema mimi ni nani?”
- 28 Wakamjibu, “Baadhi husema wewe ni Yahya, wengine husema ni Ilya, na bado wengine husema wewe ni mmoja wa manabii.”
- 29 Akawauliza, “Je, ninyi mnasema mimi ni nani?” Petro akajibu, “Wewe ndiwe Al-Masihi.”
- 30 Isa akawaonya wasimwambie mtu yeyote habari zake.
Luk 9:18–21
- 18 Siku moja Isa alipokuwa akiomba faraghani, nao wanafunzi wake wakiwa pamoja naye, akawauliza, “Watu husema mimi ni nani?”
- 19 Wakamjibu, “Baadhi husema wewe ni Yahya, wengine husema ni Ilya, na wengine husema kwamba ni mmoja wa manabii wa kale amefufuka.”
- 20 Kisha akawauliza, “Je, ninyi mnasema mimi ni nani?” Petro akajibu, “Wewe ndiwe Al-Masihi wa Mungu.”
- 21 Isa akawakataza wasimwambie mtu yeyote jambo hilo.