MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

Jairus' Daughter and the Woman Healed

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 9:18–26

  1. 18 Isa alipokuwa akiwaambia mambo haya, kiongozi wa sinagogi akaingia, akapiga magoti mbele yake, akamwambia, “Binti yangu amekufa sasa hivi. Lakini njoo uweke mkono wako juu yake, naye ataishi.”
  2. 19 Isa akaondoka akafuatana naye, nao wanafunzi wake pia wakaandamana naye.
  3. 20 Wakati huo huo, mwanamke mmoja, aliyekuwa na ugonjwa wa kutokwa damu kwa muda wa miaka kumi na mbili, akaja nyuma ya Isa, akagusa upindo wa vazi lake,
  4. 21 kwa maana alisema moyoni mwake, “Nikigusa tu vazi lake, nitaponywa.”
  5. 22 Isa akageuka, naye alipomwona akamwambia, “Binti, jipe moyo, imani yako imekuponya.” Naye yule mwanamke akapona kuanzia saa hiyo.
  6. 23 Isa alipofika nyumbani mwa yule kiongozi wa sinagogi na kuwaona waombolezaji wakipiga filimbi za maombolezo na watu wengi wakipiga kelele,
  7. 24 akawaambia, “Ondokeni! Kwa maana binti huyu hakufa, bali amelala.” Wakamcheka kwa dhihaka.
  8. 25 Lakini watu walipokwisha kutolewa nje, akaingia mle ndani na kumshika yule binti mkono, naye akaamka.
  9. 26 Habari hizi zikaenea katika maeneo yale yote.

Mrk 5:21–43

  1. 21 Isa alipokwisha kuvuka tena na kufika ng’ambo, umati mkubwa wa watu wakamzunguka hapo kando ya bahari.
  2. 22 Kisha mmoja wa viongozi wa sinagogi aliyeitwa Yairo akafika pale. Naye alipomwona Isa, akapiga magoti miguuni pake,
  3. 23 akamsihi akisema, “Binti yangu mdogo ni mgonjwa mahututi. Tafadhali nakusihi, njoo uweke mikono yako juu yake ili apate kupona, naye ataishi.”
  4. 24 Hivyo Isa akaenda pamoja naye. Umati mkubwa wa watu wakamfuata, nao watu wakawa wanamsonga.
  5. 25 Hapo palikuwa na mwanamke aliyekuwa amesumbuliwa na tatizo la kutokwa damu kwa miaka kumi na mbili.
  6. 26 Mwanamke huyu alikuwa ameteseka sana kwa mikono ya matabibu wengi, na kutumia kila kitu alichokuwa nacho. Lakini badala ya kupona, hali yake ilizidi kuwa mbaya.
  7. 27 Alikuwa amesikia habari za Isa, naye akaja kwa nyuma yake kwenye umati wa watu, akaligusa vazi lake,
  8. 28 kwa maana alisema moyoni mwake, “Nikiligusa vazi lake tu, nitaponywa.”
  9. 29 Mara kutoka damu kwake kukakoma, naye akajisikia mwilini mwake amepona kabisa.
  10. 30 Ghafula Isa akatambua kuwa nguvu zimemtoka. Akageukia umati wa watu na kuuliza, “Ni nani aliyegusa mavazi yangu?”
  11. 31 Wanafunzi wake wakamjibu, “Unaona jinsi watu wanavyokusonga. Wawezaje kuuliza, ‘Ni nani aliyenigusa?’ ”
  12. 32 Lakini Isa akaangalia pande zote ili aone ni nani aliyemgusa.
  13. 33 Yule mwanamke, akijua kilichomtokea, akaja, akaanguka miguuni pake akitetemeka kwa hofu, akamweleza ukweli wote.
  14. 34 Isa akamwambia, “Binti, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, upone kabisa ugonjwa wako.”
  15. 35 Alipokuwa bado anaongea, watu wakafika kutoka nyumbani mwa Yairo. Wakamwambia, “Binti yako amekufa. Kwa nini kuendelea kumsumbua Mwalimu?”
  16. 36 Aliposikia hayo waliyosema, Isa akamwambia huyo kiongozi wa sinagogi, “Usiogope. Amini tu.”
  17. 37 Hakumruhusu mtu yeyote amfuate isipokuwa Petro, Yakobo na Yohana, nduguye Yakobo.
  18. 38 Walipofika nyumbani mwa yule kiongozi wa sinagogi, Isa akaona ghasia, watu wakilia na kuomboleza kwa sauti kubwa.
  19. 39 Alipokwisha kuingia ndani, akawaambia, “Kwa nini mnafanya ghasia na kulia? Mtoto hajafa, bali amelala tu.”
  20. 40 Wale watu wakamcheka. Baada ya kuwafukuza wote nje, Isa akaenda na baba na mama wa yule mtoto, pamoja na wale wanafunzi aliokuwa nao, wakaingia ndani hadi pale alipokuwa mtoto yule.
  21. 41 Akamshika mtoto mkono, akamwambia, “Talitha koum!” (maana yake, “Msichana, nakuambia: amka!”)
  22. 42 Mara yule msichana akasimama, akaanza kutembea (alikuwa na umri wa miaka kumi na mbili). Walipoona haya, wakastaajabu sana.
  23. 43 Isa akawaagiza kwa ukali wasimweleze mtu yeyote jambo hilo, naye akawaambia wampe yule msichana chakula.

Luk 8:40–56

  1. 40 Basi Isa aliporudi, umati mkubwa wa watu wakampokea kwa furaha, kwani walikuwa wakimngojea.
  2. 41 Kisha mtu mmoja, jina lake Yairo, aliyekuwa kiongozi wa sinagogi, akaja na kuanguka miguuni mwa Isa, akimwomba afike nyumbani mwake,
  3. 42 kwa kuwa binti yake wa pekee, mwenye umri wa miaka kumi na mbili, alikuwa anakufa. Isa alipokuwa akienda, umati wa watu wakamsonga sana.
  4. 43 Palikuwa na mwanamke mmoja aliyekuwa na tatizo la kutokwa damu kwa muda wa miaka kumi na mbili, [na alikuwa amegharimia mali yake yote kwa matibabu] lakini hakuna yeyote aliyeweza kumponya.
  5. 44 Huyo mwanamke akaja kwa nyuma ya Isa na kugusa upindo wa vazi lake. Mara kutokwa damu kwake kukakoma.
  6. 45 Isa akauliza, “Ni nani aliyenigusa?” Watu wote walipokana, Petro akasema, “Bwana, umati huu wa watu wanakusonga na kukusukuma kila upande.”
  7. 46 Lakini Isa akasema, “Kuna mtu aliyenigusa, kwa maana nimetambua kuwa nguvu zimenitoka.”
  8. 47 Yule mwanamke alipofahamu ya kuwa hawezi kuendelea kujificha, alikuja akitetemeka, akaanguka miguuni mwa Isa. Akaeleza mbele ya watu wote kwa nini alimgusa na jinsi alivyoponywa mara moja.
  9. 48 Basi Isa akamwambia, “Binti, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani.”
  10. 49 Isa alipokuwa bado anasema, akaja mtumishi kutoka nyumbani mwa Yairo, yule kiongozi wa sinagogi, kumwambia, “Binti yako amekwisha kufa. Usiendelee kumsumbua Mwalimu.”
  11. 50 Isa aliposikia jambo hili, akamwambia Yairo, “Usiogope. Amini tu, naye binti yako atapona.”
  12. 51 Walipofika nyumbani mwa Yairo, hakumruhusu mtu yeyote aingie ndani naye isipokuwa Petro, Yohana na Yakobo, pamoja na baba na mama wa yule binti.
  13. 52 Wakati ule ule watu wote walikuwa wakilia na kuomboleza kwa ajili ya huyo binti. Isa akawaambia, “Acheni kulia. Huyu binti hajafa, ila amelala.”
  14. 53 Wao wakamcheka kwa dharau, wakijua kuwa amekwisha kufa.
  15. 54 Isa akamshika yule binti mkono na kuita, “Binti, amka!”
  16. 55 Roho yake ikamrudia, naye akainuka mara moja. Akaamuru apewe kitu cha kula.
  17. 56 Wazazi wake wakastaajabu sana, lakini Isa akawakataza wasimwambie mtu yeyote kuhusu yale yaliyotukia.