MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

Healing the Paralytic

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 9:1–8

  1. 1 Isa akaingia kwenye chombo, akavuka na kufika katika mji wa kwao.
  2. 2 Wakati huo huo wakamletea mtu aliyepooza, akiwa amelazwa kwenye mkeka. Isa alipoiona imani yao, alimwambia yule mtu aliyepooza, “Mwanangu, jipe moyo mkuu. Dhambi zako zimesamehewa.”
  3. 3 Kwa ajili ya jambo hili, baadhi ya walimu wa Torati wakasema mioyoni mwao, “Huyu mtu anakufuru!”
  4. 4 Lakini Isa akiyafahamu mawazo yao, akawaambia, “Kwa nini mnawaza maovu mioyoni mwenu?
  5. 5 Je, ni lipi lililo rahisi zaidi: kusema, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Inuka, uende’?
  6. 6 Lakini nataka mpate kujua kwamba Mwana wa Adamu ana mamlaka duniani kusamehe dhambi.” Ndipo akamwambia yule aliyepooza, “Inuka, chukua mkeka wako, uende nyumbani mwako.”
  7. 7 Yule mtu akasimama, akaenda nyumbani mwake.
  8. 8 Umati wa watu walipoyaona haya, wakajawa na hofu ya Mungu, wakamtukuza Mungu aliyekuwa amewakabidhi wanadamu mamlaka kama haya.

Mrk 2:1–12

  1. 1 Baada ya siku kadhaa Isa alirudi Kapernaumu, watu wakasikia kwamba yupo nyumbani.
  2. 2 Watu wengi wakakusanyika, kiasi kwamba hapakubaki nafasi yoyote hata mlangoni! Naye akawahubiria Neno.
  3. 3 Ndipo baadhi ya watu wakaja wakamletea Isa mtu aliyepooza, akiwa amebebwa na watu wanne.
  4. 4 Kwa kuwa hawakuweza kumfikisha kwa Isa kwa sababu ya umati wa watu, walitoboa tundu kwenye paa juu ya mahali Isa alikuwa, wakamshusha mtu aliyepooza akiwa amelalia mkeka wake.
  5. 5 Isa alipoiona imani yao, alimwambia yule mtu aliyepooza, “Mwanangu, dhambi zako zimesamehewa.”
  6. 6 Basi baadhi ya walimu wa Torati waliokuwa wameketi pale wakawaza mioyoni mwao,
  7. 7 “Kwa nini mtu huyu anasema hivi? Huyu anakufuru! Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”
  8. 8 Mara moja Isa akatambua rohoni mwake kile walichokuwa wanawaza mioyoni mwao, naye akawaambia, “Kwa nini mnawaza hivyo mioyoni mwenu?
  9. 9 Je, ni lipi lililo rahisi zaidi: kumwambia huyu aliyepooza, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Inuka, uchukue mkeka wako, uende’?
  10. 10 Lakini ili mpate kujua kwamba Mwana wa Adamu anayo mamlaka duniani ya kusamehe dhambi”: Isa akamwambia yule aliyepooza,
  11. 11 “Nakuambia, inuka, chukua mkeka wako, uende nyumbani kwako.”
  12. 12 Yule mtu aliyekuwa amepooza akasimama, akachukua mkeka wake, akatembea machoni pao wote! Jambo hili likawashangaza wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, “Hatujapata kuona jambo kama hili kamwe!”

Luk 5:17–26

  1. 17 Siku moja Isa alipokuwa akifundisha, Mafarisayo na walimu wa Torati, waliokuwa wametoka kila kijiji cha Galilaya na kutoka Yudea na Yerusalemu, walikuwa wameketi huko. Nao uweza wa Mwenyezi Mungu ulikuwa juu yake kuponya wagonjwa.
  2. 18 Wakaja watu wamembeba mgonjwa aliyepooza kwenye mkeka. Wakajaribu kumwingiza ndani ili wamweke mbele ya Isa.
  3. 19 Walipokuwa hawawezi kufanya hivyo kwa sababu ya umati wa watu, wakapanda juu ya paa, wakaondoa baadhi ya matofali, wakamteremsha yule mgonjwa kwa mkeka wake hadi katikati ya umati ule pale mbele ya Isa.
  4. 20 Isa alipoiona imani yao, akamwambia yule mgonjwa, “Rafiki, dhambi zako zimesamehewa.”
  5. 21 Mafarisayo na wale walimu wa Torati wakaanza kuuliza, “Ni nani mtu huyu anayesema maneno ya kukufuru? Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa Mungu peke yake?”
  6. 22 Isa akijua mawazo yao akawauliza, “Kwa nini mnawaza hivyo mioyoni mwenu?
  7. 23 Je, ni lipi lililo rahisi zaidi, kumwambia, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Inuka, uende’?
  8. 24 Lakini ili mpate kujua kwamba Mwana wa Adamu anayo mamlaka duniani kusamehe dhambi.” Akamwambia yule aliyepooza, “Nakuambia, inuka, chukua mkeka wako, uende nyumbani mwako.”
  9. 25 Mara yule mtu aliyekuwa amepooza akasimama mbele yao wote, akachukua mkeka wake, akaenda zake nyumbani, huku akimtukuza Mungu.
  10. 26 Kila mmoja akashangaa na kumtukuza Mungu. Wakajawa na hofu ya Mungu, wakasema, “Leo tumeona mambo ya ajabu.”