Cleansing a Leper
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 8:1–4
- 1 Isa aliposhuka kutoka mlimani, makundi ya watu wakamfuata.
- 2 Mtu mmoja mwenye ukoma akaja na kupiga magoti mbele yake, akasema, “Bwana, ukitaka, unaweza kunitakasa.”
- 3 Isa akanyoosha mkono wake akamgusa yule mtu, akamwambia, “Nataka. Takasika!” Mara yule mtu akatakasika ukoma wake.
- 4 Kisha Isa akamwambia, “Hakikisha humwambii mtu yeyote. Lakini nenda ukajioneshe kwa kuhani, na utoe sadaka aliyoamuru Musa, ili kuwa ushuhuda kwao.”
Mrk 1:40–45
- 40 Mtu mmoja mwenye ukoma alimjia Isa, akapiga magoti, akimwomba, “Ukitaka, unaweza kunitakasa.”
- 41 Isa, akiwa amejawa na huruma, akaunyoosha mkono wake akamgusa, akamwambia, “Nataka. Takasika!”
- 42 Mara ukoma ukamtoka, naye akatakasika.
- 43 Baada ya Isa kumwonya vikali, akamruhusu aende zake mara moja;
- 44 akamwambia, “Hakikisha humwambii mtu yeyote habari hizi, bali nenda ukajioneshe kwa kuhani, na ukatoe sadaka alizoagiza Musa kwa utakaso wako, ili kuwa ushuhuda kwao.”
- 45 Lakini yule mtu akaenda akaanza kutangaza habari za kuponywa kwake waziwazi. Kwa hiyo, Isa hakuweza tena kuingia katika miji waziwazi bali alikaa sehemu zisizo na watu. Hata hivyo watu wakamfuata huko kutoka kila upande.
Luk 5:12–16
- 12 Ikawa siku moja Isa alipokuwa katika mji fulani, mtu mmoja mwenye ukoma mwili mzima akamjia. Alipomwona Isa, alianguka chini hadi uso wake ukagusa ardhi, akamsihi akisema, “Bwana, ukitaka, unaweza kunitakasa.”
- 13 Isa akanyoosha mkono wake, akamgusa yule mtu, akamwambia, “Nataka. Takasika!” Na mara ukoma wake ukatakasika.
- 14 Isa akamwagiza akisema, “Usimwambie mtu yeyote, bali nenda ukajioneshe kwa kuhani na ukatoe sadaka alizoagiza Musa kwa utakaso wako, ili kuwa ushuhuda kwao.”
- 15 Lakini habari zake Isa zikazidi sana kuenea kotekote kuliko wakati mwingine wowote. Makundi makubwa ya watu walikuwa wakikusanyika ili kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao.
- 16 Lakini mara kwa mara Isa alijitenga nao ili kwenda mahali pa faragha kuomba.