MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

God's Covenant with David

Biblia Takatifu (Swahili)

2Sa 7:1–17

  1. 1 Baada ya mfalme kuingia rasmi katika jumba lake la kifalme, naye Mwenyezi Mungu akiwa amempa amani pande zote kutoka kwa adui zake,
  2. 2 akamwambia nabii Nathani, “Mimi hapa ninaishi katika jumba la kifalme la mwerezi, wakati Sanduku la Mungu limebaki katika hema.”
  3. 3 Nathani akamjibu mfalme, “Lolote ulilo nalo moyoni, endelea ukalifanye, kwa maana Mwenyezi Mungu yu pamoja nawe.”
  4. 4 Usiku ule neno la Mwenyezi Mungu likamjia Nathani, kusema:
  5. 5 “Nenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu: Je, ewe ndiwe wa kunijengea mimi nyumba ili nikae ndani yake?
  6. 6 Sijakaa ndani ya nyumba tangu siku niliyowaleta Waisraeli kutoka Misri hadi leo. Nimekuwa nikitembea kutoka mahali pamoja hadi mahali pengine na hema kama makao yangu.
  7. 7 Popote nilipotembea pamoja na Waisraeli wote, je, nimewahi kumwambia kiongozi wao yeyote niliyemwamuru kuwachunga watu wangu Israeli, “Kwa nini hujanijengea nyumba ya mwerezi?” ’
  8. 8 “Sasa basi, mwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni: Nilikutoa malishoni na kutoka kulisha mifugo, ili uwaongoze watu wangu Israeli.
  9. 9 Nimekuwa pamoja nawe popote ulipoenda, nami nimekuondolea mbali adui zako wote mbele yako. Basi nitalifanya jina lako kuwa kuu kama majina ya watu walio wakuu sana duniani.
  10. 10 Nami nitawapatia watu wangu Israeli mahali niwapande humo ili wawe na nyumbani kwao wenyewe wasisumbuliwe tena. Watu waovu hawatawatesa tena, kama walivyofanya mwanzoni,
  11. 11 na kama walivyofanya tangu mwanzo wakati nilipowaweka viongozi juu ya watu wangu Israeli. Pia nitawapa amani mbele ya adui zenu wote. “ ‘Mwenyezi Mungu akuambia kwamba Mwenyezi Mungu mwenyewe atakujengea nyumba.
  12. 12 Siku zako zitakapokwisha nawe ulale pamoja na baba zako, nitainua mzao wako aingie mahali pako, ambaye atatoka viunoni mwako, nami nitauimarisha ufalme wake.
  13. 13 Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya Jina langu, nami nitakiimarisha kiti cha ufalme wake milele.
  14. 14 Nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu. Atakapokosea nitamwadhibu kwa fimbo ya wanadamu, kwa adhabu ya kupigwa na wanadamu.
  15. 15 Lakini upendo wangu kamwe hautaondolewa kwake, kama nilivyouondoa kwa Sauli, niliyemwondoa atoke mbele yako.
  16. 16 Nyumba yako na ufalme wako utadumu milele mbele zangu, kiti chako cha utawala kitaimarishwa milele.’ ”
  17. 17 Nathani akamwarifu Daudi maneno yote ya maono haya.

1Ch 17:1–15

  1. 1 Baada ya Daudi kuingia rasmi katika jumba lake la kifalme, akamwambia nabii Nathani, “Hebu tazama, mimi ninakaa kwenye nyumba nzuri iliyojengwa kwa mwerezi, wakati Sanduku la Agano la Mwenyezi Mungu liko ndani ya hema.”
  2. 2 Nathani akamjibu Daudi, “Lolote ulilo nalo moyoni mwako litende, kwa maana Mungu yu pamoja nawe.”
  3. 3 Usiku ule neno la Mungu likamjia Nathani, kusema:
  4. 4 “Nenda ukamwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu: Wewe hutanijengea mimi nyumba ili nikae humo.
  5. 5 Mimi sijakaa ndani ya nyumba tangu siku niliyowatoa Israeli kutoka Misri hadi leo. Nimehama kutoka hema moja hadi jingine, na kutoka mahali pamoja hadi pengine.
  6. 6 Popote nilipoenda pamoja na Waisraeli wote, je, kuna wakati nilimuuliza kiongozi yeyote niliyemwagiza kuwachunga watu wangu, “Kwa nini hujanijengea nyumba ya mwerezi?” ’
  7. 7 “Sasa basi, mwambie mtumishi wangu Daudi, ‘Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni: Nilikutoa malishoni na kutoka kulisha mifugo, ili uwaongoze watu wangu Israeli.
  8. 8 Nimekuwa pamoja nawe popote ulipoenda, nami nimekuondolea mbali adui zako wote mbele yako. Basi nitalifanya jina lako kuwa kuu kama majina ya watu walio wakuu sana duniani.
  9. 9 Nami nitawapatia watu wangu Israeli mahali na nitawapa ili wawe na mahali pao wenyewe pa kuishi na wasisumbuliwe tena. Watu waovu hawatawatesa tena, kama walivyofanya mwanzoni,
  10. 10 na ambavyo wamefanya siku zote tangu nilipowachagua viongozi kwa ajili ya watu wangu Israeli. Pia nitawatiisha adui zenu wote. “ ‘Pamoja na hayo ninakuambia kwamba Mwenyezi Mungu atakujengea nyumba:
  11. 11 Siku zako zikiisha, nawe ukaenda kulala na baba zako, nitamwinua mzao wako kuwa mfalme baada yako, mmoja wa wana wako mwenyewe, nami nitauimarisha ufalme wake.
  12. 12 Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili yangu, nami nitakiimarisha kiti cha ufalme wake milele.
  13. 13 Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu. Kamwe sitaondoa upendo wangu kwake, kama nilivyouondoa kwa yule aliyekutangulia.
  14. 14 Nitamweka juu ya nyumba yangu na ufalme wangu milele; kiti chake cha utawala nitakiimarisha milele.’ ”
  15. 15 Nathani akamwarifu Daudi maneno yote ya maono haya.