MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

Feeding the Five Thousand

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 14:13–21

  1. 13 Isa aliposikia yaliyokuwa yametukia, aliondoka kwa chombo akaenda mahali pasipo na watu ili awe peke yake. Lakini watu walipopata habari, wakamfuata kwa miguu kupitia nchi kavu kutoka miji.
  2. 14 Isa alipofika kando ya bahari, aliona makundi makubwa ya watu, akawahurumia na akawaponya wagonjwa wao.
  3. 15 Ilipofika jioni, wanafunzi wake walienda kwake, wakamwambia, “Mahali hapa ni nyikani, na muda sasa umekwisha. Waage makundi ya watu ili waende zao vijijini wakajinunulie chakula.”
  4. 16 Isa akawaambia, “Hakuna sababu ya wao kuondoka. Ninyi wapeni chakula.”
  5. 17 Wakamjibu, “Tuna mikate mitano na samaki wawili tu.”
  6. 18 Akawaambia, “Nileteeni hivyo vitu hapa.”
  7. 19 Isa akaagiza umati wa watu wakae chini kwenye nyasi. Akaichukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akainua macho yake akatazama mbinguni, akavibariki na kuimega ile mikate. Kisha akawapa wanafunzi, nao wanafunzi wakawagawia ule umati.
  8. 20 Wote wakala, wakashiba. Nao wanafunzi wakakusanya vipande vilivyosalia, wakajaza vikapu kumi na viwili.
  9. 21 Idadi ya watu waliokula walikuwa wanaume wapatao elfu tano, bila kuhesabu wanawake na watoto.

Mrk 6:30–44

  1. 30 Wale mitume wakakusanyika kwa Isa na kumpa taarifa ya mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.
  2. 31 Basi kwa kuwa watu wengi mno walikuwa wakija na kutoka, hata wakawa hawana nafasi ya kula, Isa akawaambia wanafunzi wake, “Twendeni peke yetu mahali pa faragha, mpate kupumzika.”
  3. 32 Hivyo wakaondoka kwa mashua peke yao, wakaenda mahali pasipo na watu.
  4. 33 Lakini watu wengi waliowaona wakiondoka, wakawatambua, nao wakaenda haraka kwa miguu kutoka miji yote, nao wakatangulia kufika.
  5. 34 Isa alipofika kando ya bahari, aliona kundi kubwa la watu, akawahurumia kwa maana walikuwa kama kondoo wasiokuwa na mchungaji. Kwa hiyo akaanza kuwafundisha mambo mengi.
  6. 35 Mchana ulipokuwa umeendelea sana, wanafunzi wake walienda kwake, wakamwambia, “Mahali hapa ni nyikani, nazo saa zimeenda sana.
  7. 36 Waage watu ili waende mashambani na vijijini jirani, wakajinunulie chakula.”
  8. 37 Lakini Isa akawajibu, “Ninyi wapeni chakula.” Wakamwambia, “Je, twende tukanunue mikate ya dinari mia mbili ili tuwape watu hawa wale?”
  9. 38 Akawauliza, “Kuna mikate mingapi? Nendeni mkaangalie.” Walipokwisha kujua, wakarudi, wakamwambia, “Kuna mikate mitano na samaki wawili.”
  10. 39 Kisha Isa akawaamuru wawaketishe watu makundi makundi kwenye majani,
  11. 40 nao wakaketi kwenye vikundi vya watu mia mia, na wengine hamsini hamsini.
  12. 41 Isa akaichukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akainua macho yake akatazama mbinguni, akavibariki na kuimega ile mikate. Kisha akawapa wanafunzi wake ili wawagawie wale watu wote. Pia akawagawia wote wale samaki wawili.
  13. 42 Watu wote wakala, wakashiba.
  14. 43 Nao wanafunzi wake wakakusanya vipande vilivyosalia vya mikate na samaki, wakajaza vikapu kumi na viwili.
  15. 44 Idadi ya wanaume waliokula walikuwa elfu tano.

Luk 9:10–17

  1. 10 Mitume wake waliporudi, wakamweleza Isa yote waliyofanya. Kisha akaenda nao faraghani hadi mji uitwao Bethsaida.
  2. 11 Lakini umati wa watu wakafahamu alikoenda, wakamfuata. Akawakaribisha na kunena nao kuhusu ufalme wa Mungu na kuwaponya wale wote waliokuwa wanahitaji uponyaji.
  3. 12 Ilipokaribia jioni, wale mitume kumi na wawili wakaenda kwa Isa na kumwambia, “Waage watu hawa ili waende vijijini jirani na mashambani, ili wapate chakula na mahali pa kulala, kwa maana hapa tuko nyikani.”
  4. 13 Isa akawajibu, “Ninyi wapeni chakula.” Nao wakajibu, “Tuna mikate mitano na samaki wawili tu. Labda twende tukanunue chakula cha kuwatosha watu hawa wote.”
  5. 14 (Walikuwepo wanaume wapatao elfu tano.) Isa akawaambia wanafunzi wake, “Waketisheni katika vikundi vya watu hamsini hamsini.”
  6. 15 Wanafunzi wakafanya hivyo, wakawaketisha wote.
  7. 16 Isa akaichukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni, akavibariki na kuvimega. Kisha akawapa wanafunzi ili wawagawie watu.
  8. 17 Wote wakala, wakashiba. Nao wanafunzi wakakusanya vipande vilivyosalia, wakajaza vikapu kumi na viwili.

Jhn 6:1–14

  1. 1 Baada ya haya, Isa alienda ng’ambo ya Bahari ya Galilaya (ambayo pia huitwa Bahari ya Tiberia).
  2. 2 Umati mkubwa wa watu waliendelea kumfuata, kwa sababu waliona ishara nyingi za miujiza alizofanya kwa wagonjwa.
  3. 3 Kisha Isa akapanda mlimani akaketi huko pamoja na wanafunzi wake.
  4. 4 Pasaka ya Wayahudi ilikuwa imekaribia.
  5. 5 Isa alipotazama na kuona umati ule mkubwa wa watu wakimjia, akamwambia Filipo, “Tutanunua wapi mikate ili watu hawa wale?”
  6. 6 Aliuliza swali hili kumpima, kwa maana alishajua la kufanya.
  7. 7 Filipo akamjibu, “Hata fedha kiasi cha dinari mia mbili hazitoshi kununua mikate ya kuwapa watu hawa ili kila mtu apate kidogo.”
  8. 8 Mmoja wa wanafunzi wake aitwaye Andrea, ndugu yake Simoni Petro, akamwambia,
  9. 9 “Hapa kuna mvulana mmoja mwenye mikate mitano ya shayiri na samaki wawili wadogo. Lakini hivi vitatosha nini kwa watu hawa wote?”
  10. 10 Isa akasema, “Waketisheni watu chini.” Palikuwa na majani mengi katika eneo lile, nao watu wakaketi (palikuwa na wanaume wapatao elfu tano).
  11. 11 Ndipo Isa akachukua ile mikate, akamshukuru Mungu na kuwagawia wale watu waliokuwa wameketi. Akafanya vivyo hivyo na wale samaki. Kila mtu akapata kadiri alivyotaka.
  12. 12 Watu wote walipokwisha kula na kushiba, akawaambia wanafunzi wake, “Kusanyeni vipande vilivyobaki vya ile mikate, kisipotee chochote.”
  13. 13 Hivyo wakavikusanya, wakajaza vikapu kumi na viwili kwa vipande vya ile mikate mitano ya shayiri na samaki wale wawili wadogo vilivyobakishwa na waliokula.
  14. 14 Baada ya watu kuona muujiza ule Isa aliofanya, walianza kusema, “Hakika huyu ndiye Nabii ajaye ulimwenguni!”