MEGA.Bible ค้นหา
ไทย

David's Census and the Plague

Biblia Takatifu (Swahili)

2Sa 24:1–25

  1. 1 Hasira ya Mwenyezi Mungu ikawaka tena dhidi ya Israeli, naye akamchochea Daudi dhidi yao, akisema, “Nenda ukawahesabu Israeli na Yuda.”
  2. 2 Kwa hiyo mfalme akamwambia Yoabu, pamoja na majemadari wa jeshi aliokuwa nao, “Nendeni kwa makabila yote ya Israeli kuanzia Dani hadi Beer-Sheba na mwandikishe wapiganaji, ili niweze kujua idadi yao.”
  3. 3 Lakini Yoabu akamjibu mfalme, “Mwenyezi Mungu, Mungu wako, na azidishe jeshi mara mia, nayo macho ya bwana wangu mfalme na yaone hili. Lakini kwa nini bwana wangu mfalme anataka kufanya kitu cha namna hii?”
  4. 4 Hata hivyo, neno la mfalme likawa na nguvu juu ya Yoabu pamoja na majemadari wa jeshi; kwa hiyo wakaondoka mbele ya mfalme kuandikisha wapiganaji wa Israeli.
  5. 5 Baada ya kuvuka Yordani, walipiga kambi karibu na Aroeri, kusini mwa mji ulioko kwenye bonde jembamba, ndipo wakipitia Gadi, wakaenda hadi Yazeri.
  6. 6 Walienda hadi Gileadi na pia eneo la Tahtimu-Hodshi, wakaendelea hadi Dani-Yaani na kuzunguka kuelekea Sidoni.
  7. 7 Kisha wakaelekea ngome ya Tiro pamoja na miji yote ya Wahivi na ya Wakanaani. Mwishoni, walienda Beer-Sheba katika Negebu ya Yuda.
  8. 8 Baada ya kupita katika nchi nzima, walirudi Yerusalemu baada ya miezi tisa na siku ishirini.
  9. 9 Yoabu akamtolea mfalme idadi ya wapiganaji: Katika Israeli kulikuwa wanaume wenye uwezo elfu mia nane ambao wangeweza kutumia upanga, na katika Yuda watu elfu mia tano.
  10. 10 Dhamiri ya Daudi ilishtuka baada ya kuwahesabu wapiganaji, naye akamwambia Mwenyezi Mungu, “Nimefanya dhambi kubwa kwa kufanya jambo hili. Ee Mwenyezi Mungu, sasa ninakusihi, ondoa hatia ya mtumishi wako. Nimefanya jambo la kipumbavu sana.”
  11. 11 Kabla Daudi hajaamka kesho yake asubuhi, neno la Mwenyezi Mungu lilikuwa limemjia Gadi nabii, aliyekuwa mwonaji wa Daudi, kusema:
  12. 12 “Nenda ukamwambie Daudi, ‘Hivi ndivyo asemavyo Mwenyezi Mungu: Ninakupa wewe uchaguzi wa mambo matatu. Nichagulie mojawapo nitakalotenda dhidi yako.’ ”
  13. 13 Basi Gadi akaenda kwa Daudi na kumwambia, “Je, ije njaa ya miaka mitatu katika nchi yako? Au miezi mitatu ya kukimbia adui zako wakikufuatia? Au siku tatu za tauni katika nchi yako? Basi sasa, fikiri juu ya hilo na uamue jinsi nitakavyomjibu huyo aliyenituma.”
  14. 14 Daudi akamjibu Gadi, “Nitataabika sana. Afadhali tuangukie mikononi mwa Mwenyezi Mungu, kwa maana rehema zake ni kuu, lakini usiniache nianguke mikononi mwa wanadamu.”
  15. 15 Basi Mwenyezi Mungu akatuma tauni katika Israeli kuanzia asubuhi hadi muda ulioamriwa, wakafa watu elfu sabini kuanzia Dani hadi Beer-Sheba.
  16. 16 Malaika aliponyoosha mkono wake ili kuangamiza Yerusalemu, Mwenyezi Mungu akahuzunika kwa sababu ya maafa, akamwambia yule malaika aliyekuwa anawadhuru watu, “Yatosha! Rudisha mkono wako.” Wakati huo malaika wa Mwenyezi Mungu alikuwa kwenye sakafu ya kupuria ya Arauna Myebusi.
  17. 17 Ikawa Daudi alipomwona huyo malaika aliyekuwa akiwaua watu, akamwambia Mwenyezi Mungu, “Mimi ndiye niliyetenda dhambi na kukosa. Hawa ni kondoo tu. Wamefanya nini? Mkono wako uwe juu yangu na nyumba yangu.”
  18. 18 Siku hiyo Gadi akamwendea Daudi na kumwambia, “Panda ukamjengee Mwenyezi Mungu madhabahu kwenye sakafu ya kupuria ya Arauna Myebusi.”
  19. 19 Kwa hiyo Daudi akakwea kama vile Mwenyezi Mungu alivyokuwa ameamuru kwa kinywa cha Gadi.
  20. 20 Arauna alipotazama na kumwona mfalme na maafisa wake wakija kumwelekea, alitoka nje na kusujudu, uso wake ukagusa chini mbele ya mfalme.
  21. 21 Arauna akasema, “Mbona bwana wangu mfalme amekuja kwa mtumishi wake?” Daudi akajibu, “Nimekuja kununua sakafu yako ya kupuria, niweze kumjengea Mwenyezi Mungu madhabahu, ili tauni iliyo katika watu iondolewe.”
  22. 22 Arauna akamwambia Daudi, “Bwana wangu mfalme na achukue chochote kinachompendeza na akitoe sadaka. Hapa kuna maksai kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa, pia kuna miti ya kupuria na nira za ng’ombe kwa ajili ya kuni.
  23. 23 Ee mfalme, Arauna anatoa vyote hivi kwa mfalme.” Pia Arauna akamwambia mfalme, “Mwenyezi Mungu, Mungu wako, na akukubali.”
  24. 24 Lakini mfalme akamjibu Arauna, “La hasha! Nasisitiza kuvilipia. Sitatoa sadaka ya kuteketezwa kwa Mwenyezi Mungu, Mungu wangu, isiyonigharimu chochote.” Kwa hiyo Daudi akanunua ile sakafu ya kupuria nafaka na maksai, akazilipia shekeli hamsini za fedha.
  25. 25 Kisha Daudi akamjengea Mwenyezi Mungu madhabahu mahali hapo, na kutoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Kisha Mwenyezi Mungu akajibu kwa ajili ya nchi, nayo tauni ikakoma katika Israeli.

1Ch 21:1–27

  1. 1 Shetani akainuka dhidi ya Israeli na kumshawishi Daudi ahesabu Waisraeli.
  2. 2 Kwa hiyo, Daudi akamwambia Yoabu na majemadari wa jeshi, “Nendeni mkawahesabu Waisraeli kuanzia Beer-Sheba hadi Dani. Kisha mniletee taarifa niweze kufahamu wako wangapi.”
  3. 3 Yoabu akajibu, “Mwenyezi Mungu na aongeze jeshi lake mara mia na zaidi. Mfalme bwana wangu, kwani hawa wote si raia wa bwana wangu? Kwa nini bwana wangu unataka kufanya hivi? Kwa nini kuleta hatia juu ya Israeli?”
  4. 4 Hata hivyo, neno la mfalme likawa na nguvu juu ya Yoabu; kwa hiyo Yoabu akaondoka na kuzunguka Israeli yote, kisha akarudi Yerusalemu.
  5. 5 Yoabu akamtolea Daudi idadi ya wapiganaji: Katika Israeli yote kulikuwa na watu milioni moja na elfu mia moja ambao wangeweza kutumia upanga, wakiwemo watu elfu mia nne sabini wa Yuda.
  6. 6 Lakini Yoabu hakuwahesabu Walawi na Wabenyamini, kwa sababu alichukizwa sana na amri ya mfalme.
  7. 7 Amri hii ilikuwa mbaya machoni pa Mungu pia; hivyo akaiadhibu Israeli.
  8. 8 Kisha Daudi akamwambia Mungu, “Nimetenda dhambi kubwa kwa kufanya jambo hili. Sasa, ninakusihi, ondoa hatia ya mtumishi wako. Nimefanya jambo la kipumbavu sana.”
  9. 9 Mwenyezi Mungu akamwambia Gadi, mwonaji wa Daudi,
  10. 10 “Nenda ukamwambie Daudi, hivi ndivyo asemavyo Mwenyezi Mungu: ‘Ninakupa wewe uchaguzi wa mambo matatu. Nichagulie mojawapo nitakalotenda dhidi yako.’ ”
  11. 11 Kwa hiyo Gadi akamwendea Daudi akamwambia, “Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu: ‘Chagua:
  12. 12 miaka mitatu ya njaa; au miezi mitatu ya kushindwa na adui zako, ukipatwa na panga zao; au siku tatu za upanga wa Mwenyezi Mungu: siku tatu za tauni katika nchi na malaika wa Mwenyezi Mungu akiangamiza kila mahali katika Israeli.’ Sasa basi, amua jinsi nitakavyomjibu yeye aliyenituma.”
  13. 13 Daudi akamwambia Gadi, “Ninayo mahangaiko makubwa. Mimi na nianguke mikononi mwa Mwenyezi Mungu, kwa maana rehema zake ni kuu mno, lakini usiniache niangukie mikononi mwa wanadamu.”
  14. 14 Basi Mwenyezi Mungu akatuma tauni katika Israeli, na wanaume elfu sabini wa Israeli wakafa.
  15. 15 Mungu akapeleka malaika kuangamiza Yerusalemu. Lakini malaika alipokuwa akifanya hivyo, Mwenyezi Mungu akaona na akahuzunika kwa sababu ya maafa, akamwambia yule malaika aliyekuwa anaangamiza watu, “Yatosha! Rudisha mkono wako.” Wakati huo malaika wa Mwenyezi Mungu alikuwa amesimama katika sakafu ya kupuria nafaka ya Arauna Myebusi.
  16. 16 Daudi akayainua macho yake, akamwona huyo malaika wa Mwenyezi Mungu akiwa amesimama katikati ya mbingu na dunia, naye ameunyoosha upanga wake juu ya Yerusalemu tayari kuangamiza. Kisha Daudi na wazee, waliokuwa wamevaa gunia, wakaanguka kifudifudi.
  17. 17 Daudi akamwambia Mungu, “Je, si mimi ndiye niliyeamuru watu wahesabiwe? Mimi ndiye niliyetenda dhambi na kukosa. Hawa ni kondoo tu. Wamefanya nini? Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu, mkono wako na uwe juu yangu na jamaa yangu, lakini usiache tauni hii iendelee juu ya watu wako.”
  18. 18 Kisha malaika wa Mwenyezi Mungu akamwamuru Gadi amwambie Daudi apande na kumjengea Mwenyezi Mungu madhabahu kwenye sakafu ya kupuria nafaka ya Arauna Myebusi.
  19. 19 Kwa hiyo Daudi akakwea, akalitii lile neno ambalo Gadi alikuwa amelisema katika jina la Mwenyezi Mungu.
  20. 20 Arauna alipokuwa akipura ngano, akageuka, akamwona yule malaika. Wanawe wanne waliokuwa pamoja naye wakajificha.
  21. 21 Kisha Daudi akakaribia, Arauna alipotazama na kumwona, akaondoka kwenye uwanja wa kupuria nafaka akamsujudia Daudi, uso wake ukagusa chini.
  22. 22 Daudi akamwambia Arauna, “Nipatie huu uwanja wako wa kupuria nafaka, niweze kujenga madhabahu ya Mwenyezi Mungu, ili tauni ipate kukomeshwa katika watu. Niuzie kwa bei yake kamili.”
  23. 23 Arauna akamwambia Daudi, “Uchukue huo uwanja. Mfalme bwana wangu na afanye lolote analopenda. Tazama, nitatoa maksai kwa ajili ya sadaka za kuteketezwa, vifaa vya kupuria kuwa kuni, pamoja na ngano kwa ajili ya dhabihu ya nafaka. Natoa hivi vyote.”
  24. 24 Lakini Mfalme Daudi akamjibu Arauna, “La hasha! Lakini ninasisitiza kwamba nitalipa bei yake kamili. Sitachukua kilicho chako kwa ajili ya Mwenyezi Mungu au kutoa sadaka ya kuteketezwa isiyonigharimu chochote.”
  25. 25 Basi Daudi akamlipa Arauna shekeli mia sita za dhahabu kwa ajili ya ule uwanja.
  26. 26 Kisha Daudi akamjengea Mwenyezi Mungu madhabahu mahali hapo, na kutoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Akamwita Mwenyezi Mungu naye Mwenyezi Mungu akajibu maombi yake kwa moto kutoka mbinguni juu ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa.
  27. 27 Kisha Mwenyezi Mungu akanena na yule malaika, naye akarudisha upanga wake katika ala yake.