Zaburi 137

1 Kando ya mito ya Babeli tuliketi, tukaomboleza tulipokumbuka Sayuni.

2 Kwenye miti ya huko tulitundika vinubi vyetu,

3 kwa maana huko hao waliotuteka walitaka tuwaimbie nyimbo; watesi wetu walidai nyimbo za furaha; walisema, “Tuimbieni wimbo mmoja kati ya nyimbo za Sayuni!”

4 Tutaimbaje nyimbo za Mwenyezi Mungu, tukiwa nchi ya kigeni?

5 Nikikusahau wewe, ee Yerusalemu, basi mkono wangu wa kuume na usahau ujuzi wake.

6 Ulimi wangu ushikamane na kaakaa la kinywa changu kama sitakukumbuka wewe, kama nisipokufikiri Yerusalemu kuwa furaha yangu kubwa.

7 Kumbuka, Ee Mwenyezi Mungu, walichokifanya Waedomu, siku ile Yerusalemu ilipoanguka. Walisema, “Bomoa, bomoa hata misingi yake!”

8 Ee binti Babeli, uliyehukumiwa kuangamizwa, heri yeye atakayekulipiza wewe kwa yale uliyotutenda sisi:

9 yeye ambaye atawakamata watoto wako wachanga na kuwaponda juu ya miamba.