Zaburi 130

1 Kutoka vilindini ninakulilia, Ee Mwenyezi Mungu.

2 Ee Bwana, sikia sauti yangu. Masikio yako na yawe masikivu kwa kilio changu unihurumie.

3 Kama wewe, Ee Mwenyezi Mungu, ungeweka kumbukumbu ya dhambi, Ee Bwana, ni nani angeweza kusimama?

4 Lakini kwako kuna msamaha, kwa hiyo wewe unaogopwa.

5 Namngojea Mwenyezi Mungu, nafsi yangu inangojea, katika neno lake naweka tumaini langu.

6 Nafsi yangu inamngojea Bwana kuliko walinzi waingojeavyo asubuhi, naam, kuliko walinzi waingojeavyo asubuhi.

7 Ee Israeli, mtumaini Mwenyezi Mungu, maana kwa Mwenyezi Mungu kuna upendo usiokoma, na kwake kuna ukombozi kamili.

8 Yeye mwenyewe ataikomboa Israeli kutoka dhambi zao zote.