Ezekieli 4
1 “Mwanadamu, sasa chukua tofali, uliweke mbele yako na uchore juu yake ramani ya mji wa Yerusalemu.
2 Kisha uuzingire: Njenga husuru dhidi yake, na upandishe kilima hadi kuta zake, weka kambi dhidi yake pande zote, pamoja na magogo ya kubomoa.
3 Kisha chukua bamba la chuma, ukalisimamishe liwe kama ukuta wa chuma kati yako na huo mji, nawe uuelekeze uso wako. Huo mji utakuwa katika hali ya kuzingirwa, nawe ndiwe utakayeuzingira. Hii itakuwa ishara kwa nyumba ya Israeli.
4 “Kisha ulale kwa upande wako wa kushoto na uweke dhambi za nyumba ya Israeli juu yako. Utazibeba dhambi zao kwa idadi ya siku utakazolala kwa huo upande mmoja.
5 Nimekupangia idadi ya siku kama miaka ya dhambi yao. Kwa hiyo kwa siku mia tatu na tisini (390), utabeba dhambi za nyumba ya Israeli.
6 “Baada ya kumaliza hili, lala chini tena, wakati huu ulale chini kwa upande wa kuume, uchukue dhambi za nyumba ya Yuda. Nimekupangia siku arobaini, siku moja kwa kila mwaka.
7 Geuza uso wako uuelekeze Yerusalemu uone jinsi ulivyozingirwa, na kwa mkono wako usiovikwa nguo, tabiri dhidi yake.
8 Nitakufunga kwa kamba ili usiweze kugeuka kutoka upande mmoja hadi upande mwingine, hata utakapotimiza siku za kuzingirwa kwako.
9 “Chukua ngano na shayiri, maharagwe na dengu, mtama na mawele, uviweke na kuvihifadhi vyote kwenye gudulia la kuhifadhia, na uvitumie kujitengenezea mkate. Utaula mkate huo kwa hizo siku mia tatu na tisini (390) utakazokuwa umelala kwa upande mmoja.
10 Pima shekeli ishirini za chakula utakachokula kwa kila siku, nawe utakula kwa wakati uliopangwa.
11 Pia pima maji sehemu ya sita ya hini, nawe utakunywa kwa wakati uliopangwa.
12 Nawe utakula chakula vile ungekula mkate wa shayiri; uoke mkate mbele ya macho ya watu, ukitumia moto wa kinyesi cha mwanadamu.”
13 Mwenyezi Mungu akasema, “Hivi ndivyo watu wa Israeli watakavyokula chakula kilicho najisi miongoni mwa mataifa ninakowapeleka.”
14 Ndipo nikasema, “Sivyo Bwana Mungu Mwenyezi! Kamwe mimi sijajitia unajisi. Tangu ujana wangu hadi sasa sijala kamwe kitu chochote kilichokufa au kilichoraruliwa na wanyama pori. Hakuna nyama yoyote najisi iliyoingia kinywani mwangu.”
15 Akasema, “Vema sana, basi nitakuruhusu uoke mkate wako kwa kutumia kinyesi cha ng’ombe badala ya kinyesi cha mwanadamu.”
16 Kisha Mungu akaniambia, “Mwanadamu! Mimi nitasababisha uhaba wa chakula katika Yerusalemu. Watu watakula chakula cha mgawo kwa wasiwasi, na maji ya mgawo kwa kukata tamaa,
17 kwa kuwa chakula na maji vitakuwa adimu. Kila mmoja atastaajabu kumwona mwenzake, nao watadhoofika kwa sababu ya dhambi yao.
Cross-references
78
- 1Hos 1:2–9, Hos 12:10, Jer 18:2–12, Amo 3:2, 1Ki 11:30–31, Hos 3:1–5, 1Sa 15:27–28, Jer 27:2–22
- 2Ezk 21:22, Jer 6:6, Luk 19:42–44, Jer 39:1–2, Jer 52:4
- 3Isa 8:18, Ezk 12:6, Isa 20:3, Ezk 12:11, Ezk 24:24–27, Lev 2:5, Heb 2:4, Jer 39:1
- 4Lev 16:22, Ezk 4:8, Lev 10:17, Num 18:1, Isa 53:11–12, Mat 8:17, 2Ki 17:21–23, Ezk 4:5
- 5Num 14:34, Isa 53:6
- 6Num 14:34, Dan 9:24–26, Dan 12:11–12, Rev 11:2–3, Rev 13:5, Rev 9:15, Rev 12:14
- 7Isa 52:10, Ezk 21:2, Ezk 6:2, Ezk 4:3
- 8Ezk 3:25
- 9Ezk 4:13, Isa 28:25, Ezk 4:16
- 10Lev 26:26, Deu 28:51–68, Ezk 14:13, Isa 3:1, Ezk 45:12, Ezk 4:16
- 11Ezk 4:16, Jhn 3:34, Isa 5:13
- 12Isa 36:12, Gen 18:6
- 13Dan 1:8, Hos 9:3–4
- 14Act 10:14, Deu 14:3, Ezk 20:49, Ezk 9:8, Lev 17:15, Isa 65:4, Jer 1:6, Exo 22:31
- 16Ezk 5:16, Isa 3:1, Lev 26:26, Psa 105:16, Ezk 4:10–11, Ezk 12:18–19, Ezk 14:13, Lam 1:11
- 17Lev 26:39, Ezk 24:23, Ezk 33:10