Zaburi 149
1 Msifuni Mwenyezi Mungu. Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya, sifa zake katika kusanyiko la watakatifu.
2 Israeli na washangilie katika Muumba wao, watu wa Sayuni na wafurahi katika Mfalme wao.
3 Na walisifu jina lake kwa kucheza na wampigie muziki kwa matari na kinubi.
4 Kwa maana Mwenyezi Mungu anapendezwa na watu wake, anawavika wanyenyekevu taji la wokovu.
5 Watakatifu washangilie katika heshima hii, na waimbe kwa shangwe vitandani mwao.
6 Sifa za Mungu na ziwe vinywani mwao na upanga ukatao kuwili mikononi mwao,
7 ili walipize mataifa kisasi na adhabu juu ya mataifa,
8 wawafunge wafalme wao kwa minyororo, wakuu wao kwa pingu za chuma,
9 ili kuwafanyia hukumu iliyoandikwa dhidi yao. Huu ndio utukufu wa watakatifu wake wote. Msifuni Mwenyezi Mungu.