MEGA.Bible Suchen
Deutsch

The Last Supper

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 26:26–30

  1. 26 Walipokuwa wanakula, Isa akachukua mkate, akashukuru, akaumega, na kuwapa wanafunzi wake, akisema, “Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu.”
  2. 27 Kisha akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, “Nyweni nyote katika kikombe hiki.
  3. 28 Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.
  4. 29 Lakini ninawaambia, tangu sasa sitakunywa tena katika uzao huu wa mzabibu, hadi siku ile nitakapounywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.”
  5. 30 Walipokwisha kuimba wimbo, wakatoka wakaenda Mlima wa Mizeituni.

Mrk 14:22–26

  1. 22 Walipokuwa wanakula, Isa akachukua mkate, akashukuru, akaumega na kuwapa wanafunzi wake, akisema, “Twaeni mle; huu ndio mwili wangu.”
  2. 23 Kisha akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, nao wote wakanywa kutoka humo.
  3. 24 Akawaambia, “Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi.
  4. 25 Amin, nawaambia, sitakunywa tena katika uzao wa mzabibu, hadi siku ile nitakapounywa mpya katika ufalme wa Mungu.”
  5. 26 Walipokwisha kuimba wimbo, wakatoka wakaenda Mlima wa Mizeituni.

Luk 22:14–23

  1. 14 Wakati ulipowadia, Isa akaketi mezani pamoja na wale mitume wake.
  2. 15 Kisha akawaambia, “Nimetamani sana kuila Pasaka hii pamoja nanyi kabla ya kuteswa kwangu.
  3. 16 Kwa maana, nawaambia, sitaila tena Pasaka hadi itakapotimizwa katika ufalme wa Mungu.”
  4. 17 Baada ya kukichukua kikombe, akashukuru, akasema, “Chukueni hiki mnywe wote.
  5. 18 Kwa maana nawaambia tangu sasa sitakunywa tena katika uzao wa mzabibu, hadi ufalme wa Mungu utakapokuja.”
  6. 19 Kisha akachukua mkate, akashukuru, akaumega, na kuwapa, akisema, “Huu ni mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu. Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.”
  7. 20 Vivyo hivyo baada ya kula, akakitwaa kikombe, akisema, “Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, imwagikayo kwa ajili yenu.
  8. 21 Lakini mkono wake huyo atakayenisaliti uko hapa mezani pamoja nami.
  9. 22 Mwana wa Adamu anaenda zake kama ilivyokusudiwa. Lakini ole wake mtu huyo amsalitiye!”
  10. 23 Wakaanza kuulizana wenyewe ni nani miongoni mwao angeweza kufanya jambo hilo.