The Last Supper
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 26:26–30
- 26 Walipokuwa wanakula, Isa akachukua mkate, akashukuru, akaumega, na kuwapa wanafunzi wake, akisema, “Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu.”
- 27 Kisha akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, “Nyweni nyote katika kikombe hiki.
- 28 Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.
- 29 Lakini ninawaambia, tangu sasa sitakunywa tena katika uzao huu wa mzabibu, hadi siku ile nitakapounywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.”
- 30 Walipokwisha kuimba wimbo, wakatoka wakaenda Mlima wa Mizeituni.
Mrk 14:22–26
- 22 Walipokuwa wanakula, Isa akachukua mkate, akashukuru, akaumega na kuwapa wanafunzi wake, akisema, “Twaeni mle; huu ndio mwili wangu.”
- 23 Kisha akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, nao wote wakanywa kutoka humo.
- 24 Akawaambia, “Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi.
- 25 Amin, nawaambia, sitakunywa tena katika uzao wa mzabibu, hadi siku ile nitakapounywa mpya katika ufalme wa Mungu.”
- 26 Walipokwisha kuimba wimbo, wakatoka wakaenda Mlima wa Mizeituni.
Luk 22:14–23
- 14 Wakati ulipowadia, Isa akaketi mezani pamoja na wale mitume wake.
- 15 Kisha akawaambia, “Nimetamani sana kuila Pasaka hii pamoja nanyi kabla ya kuteswa kwangu.
- 16 Kwa maana, nawaambia, sitaila tena Pasaka hadi itakapotimizwa katika ufalme wa Mungu.”
- 17 Baada ya kukichukua kikombe, akashukuru, akasema, “Chukueni hiki mnywe wote.
- 18 Kwa maana nawaambia tangu sasa sitakunywa tena katika uzao wa mzabibu, hadi ufalme wa Mungu utakapokuja.”
- 19 Kisha akachukua mkate, akashukuru, akaumega, na kuwapa, akisema, “Huu ni mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu. Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.”
- 20 Vivyo hivyo baada ya kula, akakitwaa kikombe, akisema, “Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, imwagikayo kwa ajili yenu.
- 21 Lakini mkono wake huyo atakayenisaliti uko hapa mezani pamoja nami.
- 22 Mwana wa Adamu anaenda zake kama ilivyokusudiwa. Lakini ole wake mtu huyo amsalitiye!”
- 23 Wakaanza kuulizana wenyewe ni nani miongoni mwao angeweza kufanya jambo hilo.