Stilling the Storm
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 8:23–27
- 23 Naye alipoingia kwenye mashua, wanafunzi wake wakamfuata.
- 24 Ghafula, kukatokea dhoruba kali baharini hata mashua ikaanza kufunikwa na mawimbi, lakini Isa alikuwa amelala usingizi.
- 25 Wanafunzi wake wakamwendea na kumwamsha, wakisema, “Bwana, tuokoe! Tunazama!”
- 26 Naye Isa akawaambia, “Kwa nini mnaogopa, enyi wa imani haba?” Kisha akaamka na kukemea dhoruba na mawimbi, nayo bahari ikatulia kabisa.
- 27 Wale watu wakashangaa, wakisema, “Ni mtu wa namna gani huyu? Hata upepo na mawimbi vinamtii!”
Mrk 4:35–41
- 35 Ilipokaribia jioni ya siku hiyo, Isa akawaambia wanafunzi wake, “Tuvukeni hadi ng’ambo ya ziwa.”
- 36 Wakaacha umati wa watu, na wakamchukua vile alivyokuwa kwenye mashua. Palikuwa pia na mashua zingine nyingi pamoja naye.
- 37 Kukawa na dhoruba kali, nayo mawimbi yakaipiga ile mashua hata ikawa karibu kujaa maji.
- 38 Isa alikuwa katika shetri, akiwa analala juu ya mto. Wanafunzi wake wakamwamsha, wakamwambia, “Mwalimu, hujali kama tunazama?”
- 39 Akaamka, akaukemea ule upepo, akayaambia yale mawimbi, “Uwe kimya! Tulia!” Ule upepo ukatulia, kukawa shwari kabisa.
- 40 Isa akawaambia wanafunzi wake, “Kwa nini mnaogopa hivyo? Je, bado hamna imani?”
- 41 Nao wakawa wameogopa sana, wakaulizana, “Ni nani huyu? Hata upepo na mawimbi vinamtii!”
Luk 8:22–25
- 22 Siku moja Isa alipanda ndani ya mashua pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, “Tuvukeni hadi ng’ambo ya ziwa.” Nao wakaondoka.
- 23 Hivyo walipokuwa wakienda, akalala usingizi. Dhoruba kali ikatokea mle ziwani, hata mashua ikawa inajaa maji, nao walikuwa katika hatari kubwa.
- 24 Wanafunzi wake wakamwendea na kumwamsha, wakisema, “Bwana, Bwana, tunaangamia!” Yeye akaamka, akaukemea ule upepo na yale mawimbi; dhoruba ikakoma, nako kukawa shwari.
- 25 Akawauliza wanafunzi wake, “Imani yenu iko wapi?” Kwa woga na mshangao wakaulizana, “Huyu ni nani, ambaye anaamuru hata upepo na maji, navyo vikamtii?”