MEGA.Bible Suchen
Deutsch

Solomon Asks for Wisdom

Biblia Takatifu (Swahili)

1Ki 3:5–15

  1. 5 Mwenyezi Mungu akamtokea Sulemani huko Gibeoni wakati wa usiku katika ndoto, naye Mungu akasema, “Omba lolote utakalo nikupe.”
  2. 6 Sulemani akajibu, “Umemfanyia mtumishi wako, baba yangu Daudi, fadhili nyingi, kwa kuwa alikuwa mwaminifu kwako na mwenye haki, tena mnyofu wa moyo. Nawe umemzidishia fadhili hii kuu kwani umempa mwana wa kuketi kwenye kiti chake cha ufalme, kama ilivyo leo.
  3. 7 “Sasa, Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wangu, umemfanya mtumishi wako mfalme mahali pa baba yangu Daudi. Lakini mimi ni mtoto mdogo tu, wala sijui jinsi ya kutekeleza wajibu wangu.
  4. 8 Mtumishi wako yuko hapa miongoni mwa watu uliowachagua: taifa kubwa, watu wengi wasioweza kuhesabika wala kutoa idadi yao.
  5. 9 Hivyo mpe mtumishi wako moyo wa ufahamu ili kutawala watu wako na kupambanua kati ya mema na mabaya. Kwa maana, ni nani awezaye kutawala watu wako hawa walio wengi hivi?”
  6. 10 Bwana akapendezwa kwamba Sulemani ameliomba jambo hili.
  7. 11 Basi Mungu akamwambia, “Kwa kuwa umeomba neno hili na hukuomba maisha marefu au upate utajiri kwa nafsi yako, wala adui zako wafe, bali umeomba busara katika kutoa haki,
  8. 12 nitafanya uliloomba. Nitakupa moyo wa hekima na wa ufahamu, kiasi kwamba hajakuwa mtu mwingine kama wewe, wala kamwe hatakuwa baada yako.
  9. 13 Zaidi ya hayo, nitakupa yale ambayo hukuomba: utajiri na heshima; siku za maisha yako yote hapatakuwa na mtu kama wewe miongoni mwa wafalme.
  10. 14 Nawe ukienenda katika njia zangu na kutii sheria na amri zangu vile baba yako Daudi alivyofanya, nitakupa maisha marefu.”
  11. 15 Ndipo Sulemani akaamka, akatambua kuwa ilikuwa ndoto. Akarudi Yerusalemu, akasimama mbele ya Sanduku la Agano la Mwenyezi Mungu, naye akatoa dhabihu za kuteketezwa na sadaka za amani. Kisha akawafanyia watumishi wake wote karamu.

2Ch 1:7–12

  1. 7 Usiku ule Mungu akamtokea Sulemani na kumwambia, “Omba lolote utakalo nikupe.”
  2. 8 Sulemani akamjibu Mungu, “Umemwonesha baba yangu Daudi fadhili nyingi, nawe umeniweka niwe mfalme mahali pake.
  3. 9 Sasa, Bwana Mwenyezi Mungu, ahadi yako kwa baba yangu Daudi na ithibitike, kwa kuwa umenifanya mimi mfalme juu ya watu ambao ni wengi kama mavumbi ya nchi.
  4. 10 Nakuomba unipe hekima na maarifa, ili niweze kuongoza watu hawa, kwa kuwa ni nani awezaye kutawala hawa watu wako walio wengi hivi?”
  5. 11 Mungu akamwambia Sulemani, “Kwa kuwa jambo hili ndilo shauku ya moyo wako na hukuomba mali, utajiri au heshima, wala kifo kwa ajili ya adui zako, nawe kwa kuwa hukuomba maisha marefu, bali umeomba hekima na maarifa ili kuongoza watu wangu ambao nimekufanya uwe mfalme juu yao,
  6. 12 kwa hiyo utapewa hekima na maarifa. Tena nitakupa pia mali, utajiri na heshima, ambavyo hakuna mfalme yeyote kabla yako amewahi kuwa navyo, na hakuna yeyote baada yako atakayekuwa navyo.”