Hezekiah's Illness
Biblia Takatifu (Swahili)
2Ki 20:1–11
- 1 Katika siku hizo, Hezekia akaugua, naye akawa karibu kufa. Nabii Isaya mwana wa Amozi akaenda kwake na kumwambia, “Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu: Tengeneza mambo ya nyumba yako, kwa sababu utakufa, hutapona.”
- 2 Hezekia akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Mwenyezi Mungu:
- 3 “Ee Mwenyezi Mungu, kumbuka jinsi nilivyoenenda mbele zako kwa uaminifu na kujitoa kwa moyo wangu wote, na kufanya yaliyo mema machoni pako.” Naye Hezekia akalia kwa uchungu.
- 4 Kabla Isaya hajaondoka katika ua wa kati, neno la Mwenyezi Mungu likamjia, akaambiwa:
- 5 “Rudi ukamwambie Hezekia, kiongozi wa watu wangu, ‘Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu, Mungu wa baba yako Daudi: Nimeyasikia maombi yako na nimeona machozi yako; nitakuponya. Siku ya tatu kuanzia sasa utapanda kwenda katika Hekalu la Mwenyezi Mungu.
- 6 Nitakuongezea miaka kumi na tano katika maisha yako. Nami nitakuokoa wewe pamoja na mji huu kutoka mkononi mwa mfalme wa Ashuru. Nitaulinda mji huu kwa ajili yangu, na kwa ajili ya mtumishi wangu Daudi!’ ”
- 7 Kisha Isaya akasema, “Tengenezeni dawa ya kubandika ya tini.” Wakafanya hivyo na kuiweka kwenye jipu, naye akapona.
- 8 Hezekia alimuuliza Isaya, “Kutakuwa na ishara gani kwamba Mwenyezi Mungu ataniponya mimi, na kwamba nitapanda kwenda katika Hekalu la Mwenyezi Mungu siku ya tatu tangu leo?”
- 9 Isaya akajibu, “Hii ndiyo ishara ya Mwenyezi Mungu kwako kwamba Mwenyezi Mungu atafanya kile alichoahidi: Je, kivuli kiende hatua kumi mbele, au kivuli kirudi nyuma hatua kumi?”
- 10 Hezekia akasema, “Ni jambo rahisi kwa kivuli kutangulia mbele hatua kumi, kuliko kukifanya kirudi nyuma hatua kumi.”
- 11 Ndipo nabii Isaya akamwita Mwenyezi Mungu, naye Mwenyezi Mungu akakifanya kivuli kurudi nyuma hatua kumi ambazo kilikuwa kimeshuka kwenye ngazi ya Ahazi.
Isa 38:1–8
- 1 Katika siku hizo Hezekia akaugua, naye akawa karibu kufa. Nabii Isaya mwana wa Amozi akaenda kwake na kumwambia, “Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu: Tengeneza mambo ya nyumba yako, kwa sababu utakufa, hutapona.”
- 2 Hezekia akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Mwenyezi Mungu:
- 3 “Ee Mwenyezi Mungu, kumbuka jinsi nilivyoenenda mbele zako kwa uaminifu na kujitoa kwa moyo wangu wote, na kufanya yaliyo mema machoni pako.” Naye Hezekia akalia kwa uchungu.
- 4 Ndipo neno la Mwenyezi Mungu likamjia Isaya, kusema:
- 5 “Nenda ukamwambie Hezekia, ‘Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu, Mungu wa baba yako Daudi: Nimeyasikia maombi yako na nimeona machozi yako. Nitakuongezea miaka kumi na tano katika maisha yako.
- 6 Nami nitakuokoa wewe pamoja na mji huu kutoka mkononi mwa mfalme wa Ashuru. Nitaulinda mji huu.
- 7 “ ‘Hii ndiyo ishara ya Mwenyezi Mungu kwako kwamba Mwenyezi Mungu atafanya kile alichoahidi:
- 8 Nitafanya kivuli cha jua kwenye ngazi iliyojengwa na Ahazi kirudi nyuma madaraja kumi.’ ” Hivyo jua likarudi nyuma madaraja kumi ambayo lilikuwa limeshuka.