Cleansing the Temple
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 21:12–17
- 12 Isa akaingia katika eneo la Hekalu na kuwafukuza wote waliokuwa wakinunua na kuuza vitu Hekaluni. Akazipindua meza za wale waliokuwa wakibadilisha fedha, na pia viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa.
- 13 Akawaambia, “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala,’ lakini ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang’anyi.”
- 14 Vipofu na vilema wakamwendea kule Hekaluni, naye akawaponya.
- 15 Lakini viongozi wa makuhani na walimu wa Torati walipoona mambo ya ajabu aliyofanya, na kuwasikia watoto wakishangilia katika eneo la Hekalu, wakisema, “Hosana Mwana wa Daudi,” walikasirika.
- 16 Wakamuuliza Isa, “Je, unasikia hayo hawa wanayosema?” Akawajibu, “Naam; kwani hamkusoma, “ ‘Midomoni mwa watoto wachanga na wanaonyonya umeamuru sifa’?”
- 17 Akawaacha, akatoka nje ya mji, akaenda hadi Bethania, akalala huko.
Mrk 11:15–19
- 15 Walipofika Yerusalemu, Isa akaingia katika eneo la Hekalu, akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakinunua na kuuza humo. Akazipindua meza za wale waliokuwa wakibadilisha fedha, na pia viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa,
- 16 wala hakumruhusu mtu yeyote kuchukua bidhaa kupitia ukumbi wa Hekalu.
- 17 Naye alipokuwa akiwafundisha, akasema, “Je, haikuandikwa kuwa: “ ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote’? Lakini ninyi mmeifanya kuwa ‘pango la wanyang’anyi.’ ”
- 18 Viongozi wa makuhani na walimu wa Torati wakapata habari hizi, nao wakaanza kutafuta njia ya kumuua, kwa kuwa walikuwa wakimwogopa, kwa sababu umati wote walishangazwa na mafundisho yake.
- 19 Ilipofika jioni, Isa na wanafunzi wake wakatoka nje ya mji.
Luk 19:45–48
- 45 Ndipo akaingia eneo la Hekalu, akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza vitu humo.
- 46 Naye akawaambia, “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itakuwa nyumba ya sala,’ lakini ninyi mmeifanya kuwa ‘pango la wanyang’anyi.’ ”
- 47 Kila siku alikuwa akifundisha Hekaluni. Lakini viongozi wa makuhani, walimu wa Torati na viongozi wa watu walikuwa wakitafuta njia ili kumuua.
- 48 Lakini hawakupata nafasi kwa sababu watu wote walimfuata wakiyasikiliza maneno yake kwa usikivu mwingi.