MEGA.Bible Пошук
Українська

The Empty Tomb

Biblia Takatifu (Swahili)

Mat 28:1–8

  1. 1 Baada ya Sabato, alfajiri mapema siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene na yule Mariamu mwingine walienda kulitazama kaburi.
  2. 2 Ghafula, pakawa na tetemeko kubwa la ardhi, kwa sababu malaika wa Mwenyezi Mungu alishuka kutoka mbinguni, akaenda kwenye kaburi, akalivingirisha lile jiwe na kulikalia.
  3. 3 Sura ya huyo malaika ilikuwa kama umeme, na mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji.
  4. 4 Wale walinzi wa kaburi walimwogopa sana, wakatetemeka hata wakawa kama wafu.
  5. 5 Yule malaika akawaambia wale wanawake, “Msiogope, kwa maana ninajua kuwa mnamtafuta Isa aliyesulubiwa.
  6. 6 Hayupo hapa, kwa kuwa amefufuka, kama alivyosema. Njooni mpatazame mahali alipokuwa amelazwa.
  7. 7 Kisha nendeni upesi mkawaambie wanafunzi wake kwamba, ‘Amefufuka kutoka kwa wafu, naye anawatangulia kwenda Galilaya. Mtamwona huko.’ Sasa nimekwisha kuwaambia.”
  8. 8 Hivyo wale wanawake wakaondoka pale kaburini wakiwa wamejawa na hofu, lakini wakiwa na furaha nyingi. Wakaenda mbio kuwaeleza wanafunzi wake habari hizo.

Mrk 16:1–8

  1. 1 Sabato ilipomalizika, Mariamu Magdalene, Mariamu mama yake Yakobo, na Salome walinunua manukato ili wakaupake mwili wa Isa.
  2. 2 Asubuhi na mapema, siku ya kwanza ya juma, mara tu baada ya kuchomoza jua, walienda kaburini.
  3. 3 Njiani wakawa wanaulizana wao kwa wao, “Ni nani atakayetuvingirishia lile jiwe kutoka ingilio la kaburi?”
  4. 4 Lakini walipotazama, wakaona lile jiwe, ambalo lilikuwa kubwa sana, limekwisha kuvingirishwa kutoka pale penye ingilio la kaburi.
  5. 5 Walipokuwa wakiingia mle kaburini, wakamwona kijana mmoja aliyevaa joho jeupe akiwa ameketi upande wa kuume, nao wakastaajabu.
  6. 6 Yule malaika akawaambia, “Msistaajabu. Mnamtafuta Isa, Mnasiri, aliyesulubiwa. Amefufuka! Hayuko hapa. Tazameni mahali walipomlaza.
  7. 7 Lakini nendeni mkawaambie wanafunzi wake pamoja na Petro, kwamba, ‘Anawatangulia kwenda Galilaya. Mtamwona huko kama alivyowaambia.’ ”
  8. 8 Hivyo wakatoka, wakakimbia kutoka mle kaburini wakiwa na hofu kuu na mshangao. Nao hawakumwambia mtu yeyote neno lolote, kwa sababu waliogopa. Isa amtokea Mariamu Magdalene (Mathayo 28:9-10; Yohana 20:11-18) [

Luk 24:1–12

  1. 1 Siku ya kwanza ya juma, alfajiri na mapema, wale wanawake walichukua yale manukato waliyokuwa wameyaandaa, wakaenda kaburini.
  2. 2 Wakakuta lile jiwe limevingirishwa kutoka mdomo wa kaburi,
  3. 3 lakini walipoingia ndani, hawakuuona mwili wa Bwana Isa.
  4. 4 Walipokuwa wanashangaa kuhusu jambo hili, ghafula watu wawili waliokuwa wamevaa mavazi yanayong’aa kama umeme wakasimama karibu nao.
  5. 5 Wale wanawake, wakiwa na hofu, wakainamisha nyuso zao hadi chini. Lakini wale watu wakawaambia, “Kwa nini mnamtafuta aliye hai miongoni mwa wafu?
  6. 6 Hayuko hapa; amefufuka! Kumbukeni alivyowaambia alipokuwa bado yuko pamoja nanyi huko Galilaya kwamba:
  7. 7 ‘Ilikuwa lazima Mwana wa Adamu atiwe mikononi mwa watu wenye dhambi na waovu ili asulubiwe, na siku ya tatu afufuke.’ ”
  8. 8 Ndipo wakayakumbuka maneno ya Isa.
  9. 9 Waliporudi kutoka huko kaburini, wakawaeleza wale wanafunzi kumi na mmoja pamoja na wengine wote mambo haya yote.
  10. 10 Basi Mariamu Magdalene, Yoana, na Mariamu mama yake Yakobo, pamoja na wanawake wengine waliofuatana nao ndio waliwaelezea mitume habari hizi.
  11. 11 Lakini hawakuwasadiki hao wanawake, kwa sababu maneno yao yalionekana kama upuzi.
  12. 12 Hata hivyo, Petro akainuka na kukimbia kwenda kule kaburini. Alipoinama kuchungulia, akaona vile vitambaa vya kitani, ila hakuona kitu kingine. Naye akaenda zake akijiuliza nini kilichotokea.

Jhn 20:1–10

  1. 1 Alfajiri na mapema siku ya kwanza ya juma, kulipokuwa bado giza, Mariamu Magdalene alienda kaburini na kukuta lile jiwe limeondolewa penye ingilio.
  2. 2 Hivyo akakimbia kwa Simoni Petro pamoja na yule mwanafunzi mwingine ambaye Isa alimpenda, na kusema, “Wamemwondoa Bwana kaburini, na hatujui walikomweka!”
  3. 3 Petro na yule mwanafunzi mwingine wakaondoka mara moja kuelekea kaburini.
  4. 4 Wote wawili walikuwa wanakimbia, lakini yule mwanafunzi mwingine akakimbia mbio kuliko Petro, akatangulia kufika kaburini.
  5. 5 Akainama na kuchungulia mle kaburini, akaona vile vitambaa vya kitani, lakini hakuingia.
  6. 6 Ndipo Simoni Petro akaja akimfuata nyuma, akaingia ndani ya kaburi. Naye akaona vile vitambaa vya ile sanda vikiwa pale chini,
  7. 7 na kile kitambaa kilichokuwa kichwani mwa Isa. Kitambaa hicho kilikuwa kimekunjwa peke yake, mbali na vile vitambaa vya kitani vya ile sanda.
  8. 8 Kisha yule mwanafunzi aliyetangulia kufika kaburini akaingia ndani, akaona, na akaamini.
  9. 9 (Kwa kuwa hadi wakati huo walikuwa bado hawajaelewa kutoka Maandiko kwamba ilikuwa lazima Isa afufuke kutoka kwa wafu.)
  10. 10 Kisha hao wanafunzi wakaondoka, wakarudi nyumbani mwao.