Zaburi 96
1 Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya; mwimbieni Mwenyezi Mungu dunia yote.
2 Mwimbieni Mwenyezi Mungu, lisifuni jina lake; tangazeni wokovu wake siku baada ya siku.
3 Tangazeni utukufu wake katika mataifa, matendo yake ya ajabu miongoni mwa mataifa yote.
4 Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni mkuu mwenye kustahili kusifiwa kuliko wote; yeye ni wa kuogopwa kuliko miungu yote.
5 Kwa maana miungu yote ya mataifa ni sanamu, lakini Mwenyezi Mungu aliziumba mbingu.
6 Fahari na enzi viko mbele yake; nguvu na utukufu vimo patakatifu pake.
7 Mpeni Mwenyezi Mungu, enyi jamaa za mataifa, mpeni Mwenyezi Mungu utukufu na nguvu.
8 Mpeni Mwenyezi Mungu utukufu unaostahili jina lake; leteni sadaka na mje katika nyua zake.
9 Mwabuduni Mwenyezi Mungu katika uzuri wa utakatifu wake; dunia yote na itetemeke mbele zake.
10 Semeni katika mataifa kwamba, “Mwenyezi Mungu anatawala.” Ulimwengu ameuweka imara, hauwezi kusogezwa; atawahukumu watu kwa uadilifu.
11 Mbingu na zishangilie, nchi na ifurahi; bahari na ivume, na vyote vilivyo ndani yake;
12 mashamba na yashangilie, pamoja na vyote vilivyomo. Kisha miti yote ya msituni itaimba kwa furaha;
13 itaimba mbele za Mwenyezi Mungu kwa maana anakuja, anakuja kuihukumu dunia. Ataihukumu dunia kwa haki, na mataifa katika kweli yake.