Zaburi 82

1 Mungu anaongoza kusanyiko kuu, anatoa hukumu miongoni mwa “miungu”:

2 “Hata lini utaendelea kuwatetea wasio haki na kuonesha upendeleo kwa waovu?

3 Teteeni wanyonge na yatima, tunzeni haki za maskini na waliodhulumiwa.

4 Mwokoeni mnyonge na mhitaji, wakomboeni kutoka mkononi mwa mwovu.

5 “Hawajui lolote, hawaelewi lolote. Wanatembea gizani; misingi yote ya dunia imetikisika.

6 “Nilisema, ‘Ninyi ni “miungu”; ninyi nyote ni wana wa Aliye Juu Sana.’

7 Lakini mtakufa kama wanadamu wa kawaida; mtaanguka kama mtawala mwingine yeyote.”

8 Ee Mungu, inuka uihukumu nchi, kwa kuwa mataifa yote ni urithi wako.