Zaburi 131

1 Moyo wangu hauna kiburi, Ee Mwenyezi Mungu, macho yangu hayajivuni; sijishughulishi na mambo makuu kunizidi wala mambo ya ajabu mno kwangu.

2 Lakini nimetuliza na kunyamazisha nafsi yangu; kama mtoto aliyeachishwa kunyonya na mama yake, kama mtoto aliyeachishwa kunyonya ndivyo ilivyo nafsi iliyo ndani yangu.

3 Ee Israeli, mtumaini Mwenyezi Mungu tangu sasa na hata milele.