Isaya 12

1 Katika siku ile utasema: “Nitakusifu wewe, Ee Mwenyezi Mungu. Ingawa ulinikasirikia, hasira yako imegeukia mbali nawe umenifariji.

2 Hakika Mungu ni wokovu wangu; nitamtumaini wala sitaogopa. Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu, ni nguvu zangu na wimbo wangu; amekuwa wokovu wangu.”

3 Kwa furaha mtachota maji kutoka visima vya wokovu.

4 Katika siku hiyo mtasema: “Mshukuruni Mwenyezi Mungu, mliitie jina lake; julisheni miongoni mwa mataifa yale aliyoyafanya, tangazeni kuwa jina lake limetukuka.

5 Mwimbieni Mwenyezi Mungu, kwa kuwa ametenda mambo makuu, hili na lijulikane duniani kote.

6 Pazeni sauti mwimbe kwa furaha, watu wa Sayuni, kwa maana mkuu ni yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli miongoni mwenu.”