Zaburi 28
1 Ninakuita wewe, Ee Mwenyezi Mungu, Mwamba wangu; usikatae kunisikiliza. Kwa sababu ukinyamaza nitafanana na walioshuka shimoni.
2 Sikia kilio changu nikikuomba unihurumie, ninapokuita ili unisaidie, ninapoinua mikono yangu kuelekea Patakatifu pa Patakatifu pako.
3 Usiniburute pamoja na waovu, pamoja na hao watendao mabaya, ambao huzungumza na majirani zao maneno mazuri, lakini mioyoni mwao wameficha chuki.
4 Walipe sawasawa na matendo yao, sawasawa na matendo yao maovu; walipe sawasawa na kazi za mikono yao, uwalipe wanavyostahili.
5 Kwa kuwa hawaheshimu kazi za Mwenyezi Mungu, na yale ambayo mikono yake imetenda, atawabomoa na kamwe hatawajenga tena.
6 Ahimidiwe Mwenyezi Mungu, kwa maana amesikia kilio changu nikimwomba anihurumie.
7 Mwenyezi Mungu ni nguvu zangu na ngao yangu, moyo wangu umemtumaini yeye, nami nimesaidiwa. Moyo wangu unarukaruka kwa furaha nami nitamshukuru kwa wimbo.
8 Mwenyezi Mungu ni nguvu ya watu wake, ngome ya wokovu kwa mpakwa mafuta wake.
9 Waokoe watu wako na uubariki urithi wako; uwe mchungaji wao na uwabebe milele.