Zaburi 126

1 Mwenyezi Mungu alipowarejesha mateka Sayuni, tulikuwa kama watu walioota ndoto.

2 Vinywa vyetu vilijaa kicheko, ndimi zetu zilijaa nyimbo za shangwe. Ndipo iliposemwa miongoni mwa mataifa, “Mwenyezi Mungu amewatendea mambo makuu.”

3 Mwenyezi Mungu ametutendea mambo makuu, nasi tumejaa furaha.

4 Ee Mwenyezi Mungu, turejeshee watu wetu waliotekwa, kama vijito katika Negebu.

5 Wapandao kwa machozi watavuna kwa nyimbo za shangwe.

6 Yeye azichukuaye mbegu zake kwenda kupanda, huku akilia, atarudi kwa nyimbo za shangwe, akichukua miganda ya mavuno yake.