Zaburi 46
1 Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.
2 Kwa hiyo hatutaogopa, hata kama dunia ikiondolewa, na milima ianguke kilindini cha bahari,
3 hata maji yake yakinguruma na kuumuka, na milima itetemeke kwa mawimbi yake.
4 Kuna mto ambao vijito vyake vinaufurahisha mji wa Mungu, mahali patakatifu ambako Aliye Juu Sana anaishi.
5 Mungu yuko katikati yake, hautaanguka, Mungu atausaidia asubuhi na mapema.
6 Mataifa yanafanya ghasia, falme zinaanguka, yeye hupaza sauti yake, dunia ikayeyuka.
7 Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni yu pamoja nasi; Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.
8 Njooni mkaone kazi za Mwenyezi Mungu jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi.
9 Anakomesha vita hata miisho ya dunia, anakata upinde na kuvunjavunja mkuki, anateketeza ngao kwa moto.
10 “Tulieni, mjue kwamba mimi ndimi Mungu; nitatukuzwa katikati ya mataifa, nitatukuzwa katika dunia.”
11 Mwenyezi Mungu, Mungu wa majeshi ya mbinguni yu pamoja nasi; Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.