Zaburi 62

1 Nafsi yangu inapata pumziko kwa Mungu peke yake; wokovu wangu watoka kwake.

2 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu; yeye ni ngome yangu, sitatikisika kamwe.

3 Mtanishambulia hadi lini? Je, ninyi nyote mtanitupa chini: Mimi niliye kama ukuta ulioinama, kama uzio unaotikisika?

4 Walikusudia kikamilifu kumwangusha toka mahali pake pa fahari; wanafurahia uongo. Kwa vinywa vyao hubariki, lakini ndani ya mioyo yao hulaani.

5 Ee nafsi yangu, upumzike, kwa Mungu peke yake, tumaini langu latoka kwake.

6 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu; ndiye ngome yangu, sitatikisika.

7 Wokovu wangu na heshima yangu viko kwa Mungu, ndiye mwamba wangu wenye nguvu na kimbilio langu.

8 Enyi watu, mtumainini yeye wakati wote, miminieni mioyo yenu kwake, kwa kuwa Mungu ni kimbilio letu.

9 Binadamu wa ngazi ya chini ni pumzi tu, nao wa ngazi ya juu ni uongo tu; wakipimwa kwenye mizani, si chochote; wote kwa pamoja ni pumzi tu.

10 Usitumainie udhalimu, wala ujivune kwa vitu vya wizi; ingawa utajiri wako utaongezeka, usiuweke moyoni mwako.

11 Jambo moja Mungu amelisema, mambo mawili nimeyasikia: kwamba, Ee Mungu, wewe una nguvu,

12 na kwamba, Ee Bwana, wewe ni mwenye upendo. Hakika utampa kila mtu thawabu kwa kadiri ya alivyotenda.