Zaburi 125
1 Wale wamtumainio Mwenyezi Mungu ni kama Mlima Sayuni, ambao hauwezi kutikisika, bali wadumu milele.
2 Kama milima inavyozunguka Yerusalemu, ndivyo Mwenyezi Mungu anavyowazunguka watu wake sasa na hata milele.
3 Fimbo ya waovu haitadumu juu ya nchi waliyopewa wenye haki, ili wenye haki wasije wakatumia mikono yao kutenda ubaya.
4 Ee Mwenyezi Mungu, watendee mema walio wema, wale walio wanyofu wa moyo.
5 Bali wale wanaogeukia njia zilizopotoka, Mwenyezi Mungu atawafukuza pamoja na watenda maovu. Amani iwe juu ya Israeli.