The Transfiguration
Biblia Takatifu (Swahili)
Mat 17:1–8
- 1 Siku sita baada ya jambo hili, Isa akawachukua Petro, Yakobo na Yohana ndugu yake Yakobo, akawapeleka juu ya mlima mrefu peke yao.
- 2 Wakiwa huko, Isa alibadilika sura mbele yao. Uso wake ukang’aa kama jua na nguo zake zikawa nyeupe kama nuru.
- 3 Ghafula wakawatokea mbele yao Musa na Ilya, wakizungumza na Isa.
- 4 Ndipo Petro akamwambia Isa, “Bwana, ni vyema sisi tukae hapa. Ukitaka, nitafanya vibanda vitatu: kimoja chako, kingine cha Musa na kingine cha Ilya.”
- 5 Petro alipokuwa angali ananena, ghafula wingu lililong’aa likawafunika, na sauti ikatoka kwenye hilo wingu ikisema, “Huyu ni Mwanangu mpendwa. Ninapendezwa naye sana. Msikieni yeye.”
- 6 Wanafunzi waliposikia haya, wakaanguka kifudifudi, wakajawa na hofu.
- 7 Lakini Isa akaja na kuwagusa, akawaambia, “Inukeni na wala msiogope.”
- 8 Walipoinua macho yao, hawakumwona mtu mwingine yeyote isipokuwa Isa.
Mrk 9:2–8
- 2 Baada ya siku sita, Isa akawachukua Petro, Yakobo na Yohana, akawapeleka juu ya mlima mrefu, mahali walipokuwa faraghani. Huko, Isa akageuka sura mbele yao.
- 3 Mavazi yake yakawa na weupe wa kuzima macho, meupe kuliko vile mtu yeyote duniani angeweza kuyang’arisha.
- 4 Musa na Ilya wakawatokea, wakawa wanazungumza na Isa.
- 5 Petro akamwambia Isa, “Mwalimu, ni vyema sisi tukae hapa. Turuhusu tujenge vibanda vitatu: kimoja chako, kingine cha Musa na kingine cha Ilya.”
- 6 Petro hakujua aseme nini kwa maana yeye na wenzake walikuwa wameogopa sana.
- 7 Ndipo pakatokea wingu, likawafunika, nayo sauti kutoka lile wingu ikasema, “Huyu ni Mwanangu mpendwa. Msikieni yeye.”
- 8 Mara walipotazama huku na huku, hawakuona tena mtu mwingine yeyote pamoja nao isipokuwa Isa.
Luk 9:28–36
- 28 Yapata siku nane baada ya Isa kusema hayo, aliwachukua Petro, Yohana na Yakobo, akaenda nao mlimani kuomba.
- 29 Alipokuwa akiomba, sura ya uso wake ikabadilika, nayo mavazi yake yakametameta kama miali ya radi.
- 30 Ghafula wakawaona watu wawili, ndio Musa na Ilya, wakizungumza naye.
- 31 Walionekana katika utukufu wakizungumza na Isa kuhusu kifo chake ambacho kingetokea huko Yerusalemu.
- 32 Petro na wenzake walikuwa wamelala usingizi mzito. Walipoamka, wakaona utukufu wa Isa na wale watu wawili waliokuwa wamesimama pamoja naye.
- 33 Musa na Ilya walipokuwa wanaondoka, Petro akamwambia Isa, “Bwana, ni vizuri tukae hapa! Tutajenga vibanda vitatu: kimoja chako, kingine cha Musa na kingine cha Ilya.” Lakini Petro hakujua alichosema.
- 34 Alipokuwa bado anazungumza, pakatokea wingu, likawafunika, nao wakaogopa walipoingia mle kwenye wingu.
- 35 Sauti ikatoka kwenye lile wingu ikisema, “Huyu ni Mwanangu mpendwa, niliyemchagua. Msikieni yeye.”
- 36 Baada ya sauti hiyo kusema, walimkuta Isa akiwa peke yake. Wale wanafunzi wakalihifadhi jambo hili, wala kwa wakati huo hawakumwambia mtu yeyote yale waliyokuwa wameyaona.