Zaburi 70

1 Ee Mungu, ufanye haraka kuniokoa; Ee Mwenyezi Mungu, njoo hima unisaidie.

2 Wale wanaotafuta kuniua, waaibishwe na kufadhaishwa; wote wanaotamani kuangamizwa kwangu, warudishwe nyuma kwa aibu.

3 Wale wanaoniambia, “Aha! Aha!” na warudi nyuma kwa sababu ya aibu yao.

4 Lakini wote wanaokutafuta washangilie na kukufurahia, wale wanaoupenda wokovu wako siku zote waseme, “Mwenyezi Mungu ni mkuu!”

5 Lakini mimi bado ni maskini na mhitaji; Ee Mungu, unijie haraka. Wewe ndiwe msaada wangu na mwokozi wangu; Ee Mwenyezi Mungu, usikawie.