Zaburi 4

1 Nijibu nikuitapo, Ee Mungu wangu mwenye haki! Nipumzishe katika shida zangu; nirehemu, usikie ombi langu.

2 Enyi watu, mtabadilisha utukufu wangu kuwa aibu hadi lini? Mtapenda udanganyifu na kufuata miungu ya uongo hadi lini?

3 Fahamuni hakika kwamba Mwenyezi Mungu amewatenga wale wamchao kwa ajili yake; Mwenyezi Mungu atanisikia nimwitapo.

4 Katika hasira yako, usitende dhambi. Tulieni kimya mkiwa vitandani mwenu, mkiichunguza mioyo yenu.

5 Toeni dhabihu zilizo haki; mtegemeeni Mwenyezi Mungu.

6 Wengi wanauliza, “Ni nani awezaye kutuonesha jema lolote?” Ee Mwenyezi Mungu, tuangazie nuru ya uso wako.

7 Wewe umejaza moyo wangu kwa furaha kubwa kuliko watu waliopata nafaka na divai kwa wingi.

8 Nitajilaza chini na kulala kwa amani, kwa kuwa wewe peke yako, Ee Mwenyezi Mungu, waniwezesha kukaa kwa salama.