Zaburi 101

1 Nitaimba kuhusu upendo wako na haki yako; kwako wewe, Ee Mwenyezi Mungu, nitaimba sifa.

2 Nitazingatia kuishi maisha yasiyo na lawama: utakuja kwangu lini? Nitatembea nyumbani mwangu kwa moyo usio na lawama.

3 Sitaweka mbele ya macho yangu kitu kiovu. Ninayachukia matendo ya watu wasio na imani; hawatashikamana nami.

4 Moyo wa ukaidi utakuwa mbali nami; nitajitenga na kila ubaya.

5 Kila amsingiziaye jirani yake kwa siri, huyo nitamnyamazisha; mwenye macho ya dharau na moyo wa kiburi huyo sitamvumilia.

6 Macho yangu yatawaelekea waaminifu katika nchi, ili waweze kuishi pamoja nami; yeye ambaye moyo wake hauna lawama atanitumikia.

7 Mdanganyifu hatakaa nyumbani mwangu, yeye asemaye kwa uongo hatasimama mbele yangu.

8 Kila asubuhi nitawanyamazisha waovu wote katika nchi; nitamkatilia mbali kila mtenda maovu kutoka mji wa Mwenyezi Mungu.