Zaburi 8
1 Ee Mwenyezi Mungu, Bwana wetu, tazama jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani kote! Umeuweka utukufu wako juu ya mbingu.
2 Midomoni mwa watoto wachanga na wanaonyonya umeamuru sifa, kwa sababu ya watesi wako, kumnyamazisha adui na mlipiza kisasi.
3 Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota, ulizoziratibisha,
4 mwanadamu ni kitu gani hata unamfikiria, binadamu ni nani hata unamjali?
5 Umemfanya chini kidogo kuliko viumbe wa mbinguni, ukamvika taji la utukufu na heshima.
6 Umemfanya mtawala juu ya kazi za mikono yako; umeweka vitu vyote chini ya miguu yake.
7 Mifugo na makundi yote pia, naam, na wanyama wa kondeni,
8 ndege wa angani na samaki wa baharini, naam, kila kinachoogelea katika njia za bahari.
9 Ee Mwenyezi Mungu, Bwana wetu, tazama jinsi lilivyo tukufu jina lako duniani kote!