Zaburi 54
1 Ee Mungu uniokoe kwa jina lako, unifanyie hukumu kwa uwezo wako.
2 Ee Mungu, sikia maombi yangu, usikilize maneno ya kinywa changu.
3 Wageni wananishambulia, watu wakatili wanayatafuta maisha yangu, watu wasiomjali Mungu.
4 Hakika Mungu ni msaada wangu, Bwana ndiye anayenitegemeza.
5 Mabaya na yawarudie wale wanaonisingizia, kwa uaminifu wako uwaangamize.
6 Nitakutolea dhabihu za hiari; Ee Mwenyezi Mungu, nitalisifu jina lako kwa kuwa ni vyema.
7 Kwa maana ameniokoa katika shida zangu zote, na macho yangu yamewatazama adui zangu kwa ushindi.