Zaburi 141

1 Ee Mwenyezi Mungu, ninakuita, njoo kwangu hima. Sikia sauti yangu ninapokuita.

2 Maombi yangu na yafike mbele zako kama uvumba; kuinua mikono yangu juu na kuwe kama dhabihu ya jioni.

3 Ee Mwenyezi Mungu, weka mlinzi kinywani mwangu, weka ulinzi mlangoni mwa midomo yangu.

4 Usiuache moyo wangu uvutwe katika jambo baya, nisije nikashiriki katika matendo maovu pamoja na watu watendao mabaya, wala nisije nikala vyakula vyao vya anasa.

5 Mtu mwenye haki na anipige: ni jambo la huruma; na anikemee: ni mafuta kichwani mwangu. Kichwa changu hakitalikataa. Hata hivyo, maombi yangu daima ni kinyume cha watenda maovu.

6 Watawala wao watatupwa chini kutoka majabali, waovu watajifunza kwamba maneno yangu yalikuwa kweli.

7 Watasema, “Kama mtu anavyolima na kuvunja ardhi, ndivyo mifupa yetu imetawanywa kwenye mlango wa kaburi.”

8 Lakini nimekaza macho yangu kwako, Ee Bwana Mungu Mwenyezi, ndani yako nimekimbilia, usiniache nife.

9 Niepushe na mitego waliyonitegea, kutokana na mitego iliyotegwa na watenda maovu.

10 Waovu na waanguke kwenye nyavu zao wenyewe, wakati mimi ninapita salama.