Zaburi 138

1 Nitakusifu wewe, Ee Mwenyezi Mungu, kwa moyo wangu wote, mbele ya “miungu” nitaimba sifa zako.

2 Nitasujudu nikielekea Hekalu lako takatifu, nami nitalisifu jina lako kwa ajili ya upendo wako na uaminifu, kwa maana umeitukuza ahadi yako zaidi ya jina lako.

3 Nilipoita, ulinijibu; ulinifanya jasiri na mwenye moyo hodari.

4 Wafalme wote wa dunia wakusifu wewe Ee Mwenyezi Mungu, wakati wanaposikia maneno ya kinywa chako.

5 Wao na waimbe kuhusu njia za Mwenyezi Mungu, kwa maana utukufu wa Mwenyezi Mungu ni mkuu.

6 Ingawa Mwenyezi Mungu yuko juu, humwangalia mnyonge, bali mwenye kiburi yeye anamjua kutokea mbali.

7 Nijapopita katikati ya shida, wewe unayahifadhi maisha yangu, unanyoosha mkono wako dhidi ya hasira ya adui zangu, kwa mkono wako wa kuume unaniokoa.

8 Mwenyezi Mungu atatimiza kusudi lake kwangu, Ee Mwenyezi Mungu, upendo wako wadumu milele: usiziache kazi za mikono yako.