Zaburi 12
1 Mwenyezi Mungu tusaidie, kwa kuwa wacha Mungu wametoweka; waaminifu wametoweka miongoni mwa wanadamu.
2 Kila mmoja humwambia jirani yake uongo; midomo yao ya hila huzungumza kwa udanganyifu.
3 Mwenyezi Mungu na akatilie mbali midomo yote ya hila na kila ulimi uliojaa majivuno,
4 ule unaosema, “Kwa ndimi zetu tutashinda; midomo ni mali yetu, bwana wetu ni nani?”
5 “Kwa sababu wanyonge wanaonewa, na wahitaji wanalia kwa uchungu, nitainuka sasa,” asema Mwenyezi Mungu. “Nitawalinda kutokana na wale wenye nia mbaya juu yao.”
6 Maneno ya Mwenyezi Mungu ni safi, kama fedha iliyosafishwa katika tanuru, iliyosafishwa mara saba.
7 Ee Mwenyezi Mungu, utatuweka salama na kutulinda na kizazi hiki milele.
8 Watu waovu huenda wakiringa kila mahali wakati yule aliye mbaya sana ndiye anayeheshimiwa miongoni mwa watu.