Zaburi 1

1 Heri mtu yule ambaye haendi katika shauri la watu waovu, wala hasimami katika njia ya wenye dhambi, au kuketi katika baraza la wenye mizaha.

2 Bali huifurahia Torati ya Mwenyezi Mungu, naye huitafakari hiyo Torati usiku na mchana.

3 Mtu huyo ni kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao huzaa matunda kwa majira yake na majani yake hayanyauki. Lolote afanyalo hufanikiwa.

4 Sivyo walivyo waovu! Wao ni kama makapi yanayopeperushwa na upepo.

5 Kwa hiyo waovu hawatastahimili hukumu, wala wenye dhambi katika kusanyiko la wenye haki.

6 Kwa maana Mwenyezi Mungu huziangalia njia za mwenye haki, bali njia za waovu zitaangamia.