Zaburi 47
1 Pigeni makofi, enyi mataifa yote, mpigieni Mungu kelele za shangwe!
2 Jinsi gani alivyo wa kutisha, Mwenyezi Mungu Aliye Juu Sana, Mfalme mkuu juu ya dunia yote!
3 Ametiisha mataifa chini yetu, watu wengi chini ya miguu yetu.
4 Alituchagulia urithi wetu, fahari ya Yakobo, aliyempenda.
5 Mungu amepaa kwa kelele za shangwe, Mwenyezi Mungu kwa sauti za tarumbeta.
6 Mwimbieni Mungu sifa, imbeni sifa, mwimbieni sifa Mfalme wetu, imbeni sifa.
7 Kwa kuwa Mungu ni mfalme wa dunia yote, mwimbieni zaburi za sifa.
8 Mungu anayatawala mataifa, Mungu ameketi kwenye kiti chake cha enzi kitakatifu.
9 Wakuu wa mataifa wanakusanyika kama watu wa Mungu wa Ibrahimu, kwa kuwa wafalme wa dunia ni mali ya Mungu; yeye ametukuka sana.