Zaburi 110

1 Mwenyezi Mungu amwambia Bwana wangu: “Keti mkono wangu wa kuume, hadi nitakapowafanya adui zako kuwa mahali pa kuweka miguu yako.”

2 Mwenyezi Mungu ataeneza fimbo yako ya utawala yenye nguvu kutoka Sayuni; utatawala katikati ya adui zako.

3 Askari wako watajitolea kwa hiari katika siku yako ya vita. Ukiwa umevikwa fahari takatifu, kutoka tumbo la mapambazuko utapokea umande wa ujana wako.

4 Mwenyezi Mungu ameapa, naye hatabadilisha mawazo yake: “Wewe ni kuhani milele, kwa mfano wa Melkizedeki.”

5 Bwana yuko mkono wako wa kuume, atawaponda wafalme siku ya ghadhabu yake.

6 Atawahukumu mataifa, akilundika mizoga na kuwaponda watawala wa dunia nzima.

7 Atakunywa maji katika kijito kando ya njia; kwa hiyo atainua kichwa chake juu.