Zaburi 11

1 Kwa Mwenyezi Mungu ninakimbilia. Unawezaje basi kuniambia: “Ruka kama ndege utorokee kwenye mlima wako.

2 Hebu tazama, waovu wanapinda nyuta zao; wanaweka mishale kwenye nyuzi zake ili wakiwa gizani, wawapige walio wanyofu wa moyo.

3 Wakati misingi imeharibiwa, mwenye haki anaweza kufanya nini?”

4 Mwenyezi Mungu yuko ndani ya Hekalu lake takatifu; Mwenyezi Mungu yuko kwenye kiti chake cha enzi mbinguni. Huwaangalia wana wa watu, macho yake yanawachunguza.

5 Mwenyezi Mungu huwachunguza wenye haki, lakini nafsi yake inachukia waovu na wale wanaopenda mapigano.

6 Atawanyeshea waovu makaa ya moto mkali na kiberiti kinachowaka; upepo wenye joto kali ndio fungu lao.

7 Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni mwenye haki, yeye hupenda haki. Wanyofu watauona uso wake.