Ezekieli 2

1 Akaniambia, “Mwanadamu, simama kwa miguu yako nami nitasema nawe.”

2 Alipokuwa akiongea nami, Roho wa Mungu akanijia na kunisimamisha wima, nikamsikia akisema nami.

3 Akaniambia: “Mwanadamu, ninakutuma kwa Waisraeli, taifa ambalo limeniasi mimi; wao na baba zao wameniasi hadi leo.

4 Watu ninaokutuma kwao ni wakaidi na wabishi. Waambie, ‘Hivi ndivyo asemavyo Bwana Mungu Mwenyezi.’

5 Kama watasikiliza au hawatasikiliza, kwa kuwa wao ni nyumba ya uasi, watajua nabii amekuwa miongoni mwao.

6 Nawe mwanadamu, usiwaogope wao wala maneno yao. Usiogope, ijapo michongoma na miiba vinakuzunguka na unaishi katikati ya nge. Usiogope yale wasemayo wala usitishwe nao, ijapo wao ni nyumba ya uasi.

7 Lazima uwaambie maneno yangu, ikiwa watasikiliza au hawatasikiliza, kwa kuwa wao ni waasi.

8 Lakini wewe mwanadamu, sikiliza ninalokuambia. Usiasi kama hiyo nyumba ya uasi. Fungua kinywa chako na ule nikupacho.”

9 Ndipo nikatazama, nami nikaona mkono ulionyooshwa kunielekea. Nao ulikuwa na kitabu,

10 ambacho alikikunjua mbele yangu. Pande zote mbili kilikuwa kimeandikwa maneno ya maombolezo, na vilio na ole.