Zaburi 111

1 Msifuni Mwenyezi Mungu. Nitamtukuza Mwenyezi Mungu kwa moyo wangu wote, katika baraza la wanyofu na katika kusanyiko.

2 Kazi za Mwenyezi Mungu ni kuu, wote wanaopendezwa nazo huzitafakari.

3 Kazi zake zimejaa fahari na utukufu, haki yake hudumu daima.

4 Amefanya maajabu yake yakumbukwe, Mwenyezi Mungu ni mwenye neema na huruma.

5 Huwapa chakula wale wanaomcha, hulikumbuka agano lake milele.

6 Amewaonesha watu wake uwezo wa kazi zake, akiwapa nchi za mataifa mengine.

7 Kazi za mikono yake ni za uaminifu na haki, mausia yake yote ni ya kuaminika.

8 Zinadumu milele na milele, zikifanyika kwa uaminifu na unyofu.

9 Aliwapa watu wake ukombozi, aliamuru agano lake milele: jina lake ni takatifu na la kuogopwa.

10 Kumcha Mwenyezi Mungu ndicho chanzo cha hekima, wote wanaozifuata amri zake wana busara. Sifa zake zadumu milele.